GEORGE ODIWUOR Na STANLEY NGOTHO
USAFIRI umeathirika pakubwa katika vijiji viwili katika eneo la Suba, Homa Bay baada ya daraja linalounganisha maeneo hayo mawili kuharibiwa na mafuriko makubwa Jumanne asubuhi.
Wakazi wa vijiji vya Gendo na Kibwer hawawezi kusafiri kutoka upande mmoja hadi mwingine baada ya Daraja la Gendo, ambalo huviunganisha vijiji hivyo viwili kuharibika kutokana na mvua kubwa ambayo imekuwa ikinyesha katika maeneo hayo.
Miongoni mwa wale walioathiriwa ni wanafunzi kutoka Shule ya Msingi ya Gendo, kutokana na hatari zinazowakabili wanapovuka mto huo. Iliwalazimu wengi wao kurejea nyumbani na kungoja kiwango cha maji kushuka kabla ya kujaribu kuvuka tena.
Kulingana na chifu wa Kata ya Gwassi Mashariki, Andrew Ombisa, vijiji hivyo vimekumbwa na mvua kubwa katika siku chache zilizopita.
“Kulinyesha sana Jumatatu. Ndiyo mvua kubwa zaidi ambayo kijiji hiki kishawahi kushuhudia,” akasema.
Wakazi walipigwa na butwaa jana Jumanne, walipopata Daraja la Gedo lililo katika Mto Lambwe likiwa limeharibika walipokuwa wakielekea kazini. Bw Ombisa alisema kuwa maji hayo yalisomba daraja hilo hadi katika Mbuga ya Wanyama ya Rumba.
Alisema lilijengwa miaka miwili iliyopita ili kurahisisha usafiri katika vijiji hivyo.
Mbali na daraja hilo, mafuriko hayo yalisomba mimea mingi iliyopandwa majuzi mashambani katika eneo la Gwassi. Hii ni baada ya Mto Lambwe kuvunja kingo zake.
Bw Ombisa alisema afisi yake ingali kubaini kiwango cha ardhi ambacho kimeathiriwa na idadi ya wakulima wanaokadiria hasara.
“Nimewaarifu wakubwa wangu, naibu kamishna wa kaunti kuhusu mkasa huo. Watatoa ushauri kwetu,” akasema.
Wakazi walisema wataathirika sana ikiwa daraja hilo halitakarabatiwa kwa haraka.
Wakati huo huo, vijiji kadhaa katika Kaunti-ndogo ya Kajiado ya Kati vimeathiriwa vibaya na mafuriko hali ambayo imewaacha wenyeji katika njiapanda, huku mamia ya wanafunzi wakishindwa kufika katika tamasha za muziki.
Mvua hiyo ambayo ilinyesha Jumatatu usiku, ilisababisha mafuriko makubwa yaliyoyafanya madaraja kadhaa kusombwa.
Kutokana na hali hiyo, wakazi wa vijiji vya Torosei na Lorngoswa hawangeweza kufika katika mji wa Illbisil kununua vyakula na bidhaa nyingine za msingi.
Wanafunzi kutoka Shule ya Msingi ya Lorngoswa walikwama katika mji wa Illbisil baada ya kupata daraja la pekee katika mji huo likiwa limesombwa na maji.
Mwalimu mkuu wa shule hiyo, Bw Emmanuel Kasaine, aliiambia Taifa Leo kwamba motisha ya wanafunzi ilishushwa pakubwa na mafuriko hayo kwani walikuwa na matumaini makubwa ya kushiriki katika mashindano hayo.