• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 2:07 PM
Magavana wataka Inspekta Jenerali amuombe Mwangaza radhi kwa mateso

Magavana wataka Inspekta Jenerali amuombe Mwangaza radhi kwa mateso

NA DAVID MUCHUI

BARAZA la Magavana linamtaka Inspekta Jenerali wa polisi, Japhet Koome aombe msamaha kwa Gavana wa Meru Kawira Mwangaza, kutokana na kisa cha kukamatwa na maafisa wa polisi Jumatano Oktoba 18, 2023.

Taarifa ya baraza hilo iliyotumwa na Naibu Mwenyekiti Ahmed Abdullahi, imetaja kitendo hicho kama dhuluma.

Bi Mwangaza alikamatwa na polisi na kuzuiliwa kwa muda wa saa tatu, alipokuwa akiongoza mradi wa kaunti wa kupeana ng’ombe wa maziwa kwa familia moja kijijni Ruiga eneo la Imenti ya Kati.

Idara ya polisi baadaye ilitoa taarifa na kukanusha madai ya tukio hilo.

Naibu Kamanda wa Polisi Meru, Bi Gladys Rutere, alisema maafisa wake walikuwa wakitekeleza wajibu wao kutokana na mikutano ya kibinafsi ya Gavana Mwangaza.

Kulikuwepo na kioja wakati Gavana Mwangaza alikataa kuondoka kabla ya kushtakiwa ama kuombwa msamaha maafisa wa polisi.

Jumatano hiyo eneo la Imenti ya Kati, Gavana Mwangaza alikamatwa na kusukumwa kwenye karandinga la polisi kwa kile alichosema ni kusambaza ng’ombe wa maziwa katika kaunti hiyo.

Wakati wanahabari walipowasili, walimpata Bi Mwangaza akiwa kwenye karandinga la polisi katika mtaa wa Ruiga.

Inadawai kwamba gavana huyo alikamatwa kwa kuhudhuria mikutano yake ya “Okolea” ambayo ilipigwa marufuku na Waziri wa Usalama wa Ndani Kithure Kindiki.

Mwezi jana, mshikemshike pia ulishuhudiwa Igembe Kusini wakati Bi Mwangaza alipokuwa anaendesha mradi wake wa ‘Okolea’, ambapo watu kadhaa walijeruhiwa na ng’ombe aliokuwa agawanye kwa wakazi masikini kuchinjwa.

Tukio hili lilifanya Profesa Kindiki kupiga marufuku shughuli za mradi huo akisema umesababisha mgawanyiko miongoni mwa jamii ya Meru.

Mradi huo wa ‘Okolea’ unatumiwa na Bi Mwangaza kusambaza bidhaa kwa wasiojiweza.

Mnamo Jumanne Oktoba 17, 2023, madiwani wa Bunge la Kaunti ya Meru walikuwa wameanzisha tena jaribio la pili la kumng’oa mamlakani kiongozi huyo wa kaunti kwa misingi ya hoja saba.

Bunge la Kaunti hiyo lilifanya jaribio la kwanza la kumfurusha Gavana Mwangaza Disemba 14 mwaka jana kabla ya Seneti kutupilia mbali kufurushwa huko Disemba 30.

Lakini baada ya miezi kadhaa ya uhusiano wa joto-baridi, Kiongozi wa Wengi katika bunge hilo Evans Mawira aliwasilisha Jumanne asubuhi notisi ya kumng’oa mamlakani, na kumpa siku saba gavana huyo kujitetea.

Miongoni mwa mashtaka hayo ni madai ya ubadhirifu na utumizi mbaya wa pesa za kaunti, upendeleo, vitendo visivyo na heshima, dharau kwa viongozi wengine na uajiri usiofuata sheria.

  • Tags

You can share this post!

Mwanamume aliyekiri kuiba mkate na maziwa Naivas kuhukumiwa...

Korti yamwacha Mackenzie kwa mataa

T L