Na CHARLES WASONGA
JUMLA ya wafanyakazi 900 wa Mamlaka ya Usambazaji wa Dawa Nchini (KEMSA) wanakabiliwa na hatari ya kufutwa kazi katika mageuzi yanayolenga kuimarisha utendakazi wake baada ya kuzongwa na sakata ya ufisadi ya Sh7.8 bilioni.
Hata hivyo, seneta wa Narok Ledama Ole Kina alipinga mpango huo akidai ni kinyume cha sheria.
Anataka mpango huo usitishwe mara moja la sivyo awasilishe kesi kortini.
Alhamisi, bodi ya mamlaka hiyo iliamuru wafanyakazi wa ngazi ya chini kufanya kazi kutoka nyumbani kwa mwezi mmoja ili kutoa nafasi kwa maafisa wakuu wa muda kuweka misingi ya mageuzi.
Amri hiyo inaanza kutekelezwa leo Ijumaa.
Kwenye taarifa kwa vyombo vya habari Mwenyekiti wa bodi hiyo Chao Mwadime alisema mchango wa wafanyakazi hao kwa Kemsa utafuatiliwa kwa kipindi cha siku 30.
“Wasimamizi wa muda watafuatilia utendakazi wa wafanyakazi hao kwa kipindi kilichowekwa katika notisi hii. Ushauri nasaha na usaidizi hitajika wa kisaikolojia utatolewa kwa wafanyakazi wote,” Bi Mwadime akaongeza.
Mwenyekiti huyo alisema kuwa mageuzi katika Kemsa yalipendekezwa na kamati maalum iliyoteuliwa na bodi yake kuchunguza changamoto zinazoikabili na hivyo kuizuia kutekeleza majukumu yake.
“Katika ripoti yake iliyowasilishwa kwa bodi ya Kemsa, kamati hiyo ilibaini changamoto kadha zinazoizuia kutimiza mahitaji ya wateja wake. Mahitaji hayo ni kama vile dawa na bidhaa zingine za kimatibabu kwa serikali za kaunti na hospitali za rufaa,” akasema Bi Mwadime.
Mwenyekiti huyo aliongeza kuwa hali hiyo imehatarisha maisha ya Wakenya na kuhujumu mpango wa Serikali wa Afya kwa Wote ifikapo mwaka wa 2022.
“Kwa hivyo mageuzi haya yataweka msingi wa kufanikishwa kwa malengo ya Ajenda Nne Kuu za Maendeleo ya Serikali, hususan kufanikishwa kwa mipango ya Afya kwa Wote,” Bi Mwadime akaongeza.
KEMSA iligonga vichwa vya habari mwaka jana kufuatia kufichuliwa kwa sakata ya ununuzi bidhaa za kutumika kama vita dhidi ya Covid-19 kinyume cha sheria na kwa bei ya juu kupita kiasi.
Bidhaa hizo zilizojumuisha barakoa na magwanda ya kutumiwa na wahudumu wa afya kujikinga dhidi ya maambukizi (PPE) zilikuwa na thamani ya Sh7.8 bilioni.
Bunge na asasi zingine zilizochunguza sakata hiyo ziligundua kuwa zabuni ya ununuzi wa bidhaa hizo ilitolewa bila idhini ya afisi husika katika Kemsa na Wizara ya Afya.
Baadhi ya kampuni zilizopewa zabuni ya thamani ya mabilioni ya fedha hazikuwa zimehitimu wala kutimiza masharti ya sheria kuhusu ununuzi wa bidhaa za umma.
Kufuatia sakata hiyo aliyekuwa Afisa Mkuu Mtendaji wa Kemsa Jonah Manjari alisimamishwa kazi, kwa muda, kwa tuhuma za kukiuka sheria wakati wa utoaji wa zabuni za ununuzi wa bidhaa hizo za kupambana na corona.
Wengine waliosimamishwa kazi baada ya kunyoshewa kidole cha lawama katika sakata hiyo ni Mkurugenzi wa Idara ya Ununuzi Charles Juma na Mkurugenzi wa Huduma za Kibiashara Eliud Mureithi.
Maafisa hao walisimamishwa kazi bodi ya zamani ya Kemsa iliyoongozwa na aliyekuwa Naibu Spika wa Seneti Kembi Gitura “ili kutoa nafasi kwa uchunguzi wa kina”.
Lakini hadi wakati huu maafisa hao na wakuu wa kampuni zilizotajwa katika sakata hiyo hawajachukuliwa hatua zozote.
Alhamisi, Bw Ole Kina alidai kuna njama ya kuiweka KEMSA chini ya usimamizi wa jeshi, hatua ambayo alisema ni kinyume cha sheria.
“Sio haki wafanyakazi wa ngazi ya chini kufutwa kazi ili Kemsa iwekwe chini ya KDF ilhali maafisa wa waliohusika na sakata ya mabilioni ya fedha wangali wanapokea nusu ya mishahara yao,” akawaambia wanahabari katika majengo ya bunge.
“Nitatetea wafanyakazi hawa kortini ikiwa bunge halitazima hatua hii inakiuka sheria na haki za kimsingi za wafanyakazi hawa,” akaongeza.
Subscribe our newsletter to stay updated