• Nairobi
  • Last Updated May 19th, 2024 9:01 PM
Mauaji: Wapenzi wa kando washukiwa

Mauaji: Wapenzi wa kando washukiwa

Na MAUREEN ONGALA

UCHUNGUZI wa vifo vya mwanamume Mjerumani, Krabbe Dieter na mpenzi wake Mkenya, Cynthia Akinyi, umechukua mwelekeo mpya baada ya wapenzi wao wa kando kushukiwa kuhusika.

Mwili wa Dieter ulipatikana chini ya jengo la orofa tano mtaani Bamburi, Kaunti ya Mombasa mnamo Ijumaa iliyopita baada ya mwili wa Akinyi kupatikana nyumbani kwao Mtwapa, Kaunti ya Kilifi mapema Jumatano.

Imesemekana kuwa, Dieter alikuwa na mpenzi wa kando aliyekuwa akiishi Bamburi na vile vile, Akinyi, 34, alikuwa na mpenzi wake wa kando. Haya yanaaminika kuwa chanzo cha ugomvi wao.

Kamanda wa Polisi katika Kaunti ya Kilifi, Bw Nelson Taliti, alisema upelelezi bado unaendelezwa ili kubainisha ukweli.

“Imedaiwa Dieter alikuwa na mpenzi mwingine wa kike lakini bado tunafanya uchunguzi ili kubainisha alifariki vipi, kwa sababu mwili wake ulipatikana chini ya jengo la orofa tano Bamburi ukiwa na majeraha na umelowa damu,” akasema Bw Taliti.

Alisema imefichuka kwamba wapenzi hao wawili walikuwa na mazoea ya kupigana.

Kulingana naye, inachunguzwa ikiwa Dieter alijitoa uhai kwa kujirusha kutoka kwa orofa ya tano ya jengo hilo kwa sababu alijua alikuwa anatafutwa kuhusu mpenzi wake ambaye alipatikana amefariki nyumbani kwake Mtwapa.

Mwili wake ulipatikana na baadhi ya mikoba kando yake, na hivyo kuibua shaka kuhusu kama alijirusha.

“Sidhani kama alijitoa uhai, kwa sababu kama angelitaka kufanya hivyo, angejitoa uhai nyumbani kwake Mtomondoni, Mtwapa baada ya kumuua mpenzi wake lakini alikuwa ametoroka mapema asubuhi na mikoba yake,” akasema mdakuzi wetu, aliyeomba kutotajwa jina.

Alikuwa akitoroka baada ya kuhusishwa na mauaji ya Akinyi, mnamo Jumatano iliyopita.

Ilisemekana walikuwa wamezozana nyumbani kwao Mtomondoni, eneo la Kwa Chief viungani mwa mji wa Mtwapa.

“Huyo mwanamume alikuwa na mpango wa kando Bamburi na mpenzi wake alipofahamishwa kuhusu hayo ndipo wakaanza kupigana,” duru zinazofuatilia kesi hiyo zikafichulia Taifa Leo.

Duru hizo zilizidi kusema kuwa, sasa uchunguzi unataka kubainisha kama mpango huyo wa kando alihusika na kifo cha Dieter, ama kama mpenzi wa kando wa Akinyi alihusika.

  • Tags

You can share this post!

ODM yatoa onyo kwa wabunge wake kuhusu BBI

ODONGO: Rais ahakikishe miradi ya Nyanza haitelekezwi