Na FAITH NYAMAI
CHAMA cha Wazimamoto Kenya (KNFBA) kimetoa wito kwa Wizara ya Elimu kuunda kamati za kupunguza visa vya moto vinavyotokea kila mara katika shule.
Katibu mkuu wa muungano huo, Francis Liech, alisema chama hicho kimejitolea kupata suluhu ya visa vya moto ambavyo vimetokea katika zaidi ya shule 40 muhula wa pili pekee.
“Tunaomba Wizara ya Elimu iunde kamati hiyo ya kufanya uchunguzi ili kuzuia matukio kama hayo siku za usoni,” akasema Bw Liech.
Kadhalika, alisema kuwa kamati hiyo itakuwa macho na kufanya ukaguzi katika kila shule ili kubaini wanafunzi wanaopanga kutekeleza uhalifu kama huo.
“Katika baadhi ya nchi zilizoendelea, kila shule ina kamati kama hiyo ya kufanya uchunguzi wa wanaopanga kuteketeza shule. Mbona serikali yetu isiunde kamati hiyo?”alihoji.