Na RICHARD MUNGUTI
MPANGAJI alifikishwa kortini kwa kumuua Landilodi wake wakibishania viatu. Florida Nyawira, 23 alidaiwa alimdunga kisu landilodi wake Bi Esther Wainaina , mwenye umri wa miaka 42.
Nyawira mama wa mtoto mmoja mwenye umri wa miaka minne alichokozana na Esther kwa sababu ya marehemu kutoa viatu na kuweka nje ya mlangoni wake.
Ugomvi mkali ulizuka kati ya Esther na Nyawira. Hakimu mkuu mahakama ya Makadara aliombwa aamuru Nyawira azuiliwe siku 21 kuwezesha polisi kukamilisha ushahidi.
Akiwasilisha ombi la kuzuiliwa kwa Nyawira kwa siku 21, Koplo Veronicah Waithera alisema mshukiwa huyo wa mauaji atapelekwa kupimwa akili ibainike ikiwa ni timamu.
“ Naomba mahakama iamuru mshukiwa azuiliwe kwa siku 21 kuwezesha kukamilishwa kwa uchunguzi,” Koplo Waithera alimrai hakimu.
Pia mahakama ilielezwa kuwa kisu alichotumia mshukiwa kumdunga Landilodi huyo kitapelekwa katika maabara ya serikali kukaguliwa.
“Kisu alichotumia kumdunga Landilodi huyo kiliokotwa na majirani waliofika kumwokoa mhasiriwa,”Koplo Waithera alisema.
Mahakama ilielezwa mhasiriwa alipelekwa zahanati ya Jericho alikotangazwa ameaga.
Mait yake , Bi Ominde alielezwa iliondolewa na kupelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Montezuma Monalisa Nairobi.
Baada ya kupimwa akili mahakama ilielezwa faili ya mshukiwa huyo itapelekwa kwa afisi ya mkurugenzi wa mashtaka ya umma kwa ushauri zaidi.
Mshtakiwa atafunguliwa shtaka la mauaji mnamo Aprili 6, 2021.