SHANGAZI;
Kuna tabia ya mpenzi wangu inayonipa wasiwasi. Anapenda sana kutazama na kutamani wanawake wengine hata tukiwa pamoja. Nimelalamika sana lakini ameshindwa kujirekebisha.
Kuna watu wasiotosheka. Inaonekana hayo ndiyo maumbile ya mpenzi wako na huwezi kumbadilisha. Kama anamezea mate wanawake wengine mkiwa pamoja, atafanya nini akiwa peke yake? Uamuzi ni wako.
Mpenzi wangu alitoweka ghafla alipojua nina mimba yake. Alikuwa ameniahidi ndoa. Mtoto wetu sasa ana miaka mitatu na kwa muda wote huo hatujaonana wala kuwasiliana. Kuna mwanamume mwingine anayenipenda na yuko tayari kunioa.
Hali kwamba mpenzi wako alikuacha baada ya kukupa mimba ni ishara hana mapenzi ya dhati kwako. Isitoshe, hajashughulika kujua hali yako na mtoto wenu. Sidhani ana mpango wowote kuhusu maisha yenu pamoja. Msahau na uendelee na maisha yako.
Nina mpenzi ninayemwamini kwa moyo wangu wote. Lakini nimeanza kuona dalili zinazonifanya nishuku ana mwingine. Nashindwa kumuuliza sababu sina ushahidi.
Hujaeleza ni dalili gani umeona ndipo umshuku. Haitakuwa vyema kumkabili kuhusu jambo hilo kwa sababu labda si kweli. Chunguza kwanza uthibitisha.
Mpenzi wangu anataka kuonja asali lakini nimemwambia hadi atakaponioa. Anasema hawezi kuvumilia na ameniomba atafute huduma hiyo kwingine tukisubiri ndoa. Ananipenda kweli?
Hayo kamwe si mapenzi. Mwanamume anaongozwa na tamaa. Kwake kukuomba ruhusa ya kutafuta mwingine wa kukidhi tamaa yake ni kukukosea heshima. Mapenzi ya dhati yana subira. Achana naye.