NA JOSEPH NDUNDA
MAHAKAMA ya Makadara imemzuilia mwanamme mmoja aliyekiri kumchapa mpeziwe aliyekumfukuza nyumbani kwake mjini Nairobi.
Elvis Mwanza, 33, alishtakiwa mbele ya Hakimu Mwandamizi wa Makadara Bi Mary Njagi, kwamba alimshambulia Mercy Wanjiru, 40, kwenye barabara ya Mfangano mjini Nairobi, Machi 18 maka huu.
Korti iliambiwa kuwa Bi Wanjiru alikuwa akiuza matunda wakati mshtakiwa alifika kwa biashara na kula matunda bila kulipa. Alianza kuzua vurugu ya kumshambulia.
Mlalamishi alipata majeraha ya kichwa na mkono yaliyompelekea kuenda hospitalini baada ya kuokolewa na wananchi. Baadaye aliripoti tukio hilo katika kituo cha polisi cha Kamukunji.
Uchuguzi wa polisi ulionyesha kuwa wawili hao walikuwa wapenzi na awali waliishi pamoja kabla ya Bw Mwanza kukosa makao baada ya kukosana.
Bi Wanjiru alimfukuza baada ya kuachana kabla hajaamua kulipiza kisasi ili kumlazimisha akubali kumrudia.
Mahakamani, mshtakiwa alisema mlalamishi ni mkewe na wamekuwa wakipitia wakati mgumu akiongeza kuwa amekuwa akiteswa.
“Utasubiri ushahidi dhidi ya kesi yako ufikishwe mahakamani ili upate nafasi ya kujitetea. Ushahidi huo utajumulisha stakabadhi za kuonyesha Bi Wanjiru alipata matibabu,” alimkatiza Bi Njagi.
Kesi hiyo itatajwa Oktoba 26 wakati wa ushahidi kuwasilishwa mahakamani.