• Nairobi
  • Last Updated May 9th, 2024 2:36 PM
Mwili wa mwanamke wapatikana umetupwa kisimani

Mwili wa mwanamke wapatikana umetupwa kisimani

Na LAWRENCE ONGARO

POLISI wanachunguza kifo cha mwanamke kilichotokea katika kijiji cha ‘Kwa Edward’ eneo la Lari, Kaunti ya Kiambu.

Mwili wa Bi Beatrice Marigi Chege ulipatikana katika kisima nje ya nyumba yake.

Afisa mkuu wa polisi katika kaunti ndogo ya Lari, Bw Stephen Kirui alithibitisha tukio hilo lililotendeka mnamo Jumanne.

Alisema wakazi wa kijiji hicho ndio waligundua mwili wa marehemu uliokuwa umetupwa ndani ya kisima kwenye boma lake.

“Wakazi wa Lari ndio walipiga ripoti katika kituo cha Lari na kwa hivyo maafisa wa upelelezi tayari wameanza kufanya uchunguzi kubainisha kiini cha kifo cha marehemu,” alisema Bw Kirui.

Afisa huyo aliwahimiza wakazi hao kushirikiana na polisi ili uchunguzi uweze kuendelea ipasavyo.

Waliouona mwili huo wa marehemu wanasema haukuwa na majeraha yoyote.

Inadaiwa kwamba watu waliofanya kitendo hicho walibomoa nyumba yake kabla ya kumwibia vyombo vyake vilivyokuwa ndani.

“Sisi kama wakazi wa hapa tulikosa kumuona marehemu kwa siku chache na ndipo baadaye mwili wake uligunduliwa kisimani,” alisema mkazi mmoja wa kijiji hicho aliyedinda kutaja jina lake.

Tukio hilo limeacha wakazi hao na wasiwasi mwingi huku wakitaka serikali kuwapa usalama wa kutosha.

Afisa huyo alisema mwili wa marehemu ulipelekwa katika chumba cha kuhifadhi maiti cha Uplands kusubiri kufanyiwa upasuaji.

Baadhi ya wakazi waliohojiwa walisema wangetaka usalama uimarishwe vilivyo ili wasizidi kuvamiwa na wahuni wasio na huruma.

You can share this post!

Malkia Strikers warejea uwanjani kesho dhidi ya Serbia

Amonde astaafu kuchezea Kenya Shujaa ikimakiza ya tisa...