• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 8:55 AM
Ni idadi ndogo tu ya wanaojitokeza Thika kujisajili wawe wapigakura

Ni idadi ndogo tu ya wanaojitokeza Thika kujisajili wawe wapigakura

Na LAWRENCE ONGARO

HUKU uandikishaji wa wapigakura ukiendelea tangu uanze Jumatatu wiki hii, ni watu wachache wanaojitokeza katika kituo cha Huduma Centre kilichoko mjini Thika.

Baadhi ya maafisa wa kusajili wapigaji kura wakionekana kuketi bure bila cha kufanya, huku wakiwa na matumaini kwamba hatimaye watu watajitokeza kujisajili.

Kulingana na afisa msimamizi wa IEBC mjini Thika Bw Jeremiah Gatheci, ni kwamba mnamo Jumatano baadhi ya watu waliojitokeza hawakubeba vitambulisho vyao na pia walipoelezwa kuvirudia makwao, hawakuonekana tena.

“Bado wale wanaotarajia kujisajili ni wachache na ni vyema kuwahamasisha ili waelezwe umuhimu wa shughuli hii,” alisema Bw Gatheci.

Alisema licha ya kwamba IEBC inawahimiza watu kujitokeza kwa wingi kujisajili ni vyema nao viongozi kuwarai wananchi kujitokeza kwa wingi.

Bw Nduati Njuguna ambaye ni mfanyabiashara na mkazi wa Thika, aliwashauri wakazi wa Thika wajitokeza kwa wingi kujisajili ili waweze kuwachagua viongozi wanaostahili.

“Hakuna haja ya kufurika kwenye vituo vya kujiandikisha dakika ya mwisho na wakati huu kuna muda mrefu wa kujiandikisha,” alisema Bw Njuguna.

Aliwahimiza vijana kujitokeza kwa wingi ili kujiandikisha ili kuleta mabadiliko wanayotaka maishani mwao.

Bi Mary Kirika aliyewania kiti cha Mwakilishi wa Wanawake wa Kaunti ya Kiambu katika uchaguzi uliopita wa 2017, aliwahimiza vijana chipukizi kujiandikisha kwa wingi kwa huu mwezi mmoja waliopewa.

“Vijana ndio wana kura nyingi wakati huu tunapoelekea uchaguzini na kwa hivyo wasichukulie jambo hilo kwa mzaha,” alisema Bi Kirika.

Alisema wakifanya uamuzi mbaya, basi wataendelea kulalamika kila mara.

Aliwahimiza wanawake kuwarai watu kwenye familia zao wachukue kura kwa wingi ili kutumika kama silaha ya kupata viongozi wanaostahili wakati wa uchaguzi kupitia njia ya demokrasia.

Bi Gladys Chania ambaye ni mwanaharakati anayepinga matumizi ya dawa za kulevya na pombe haramu, aliwashauri vijana kutumia wingi wao kuchukua kura kwa wingi.

“Vijana wana nafasi nzuri ya kubadilisha mambo na kwa hivyo huu ndio wakati wao mzuri wa kujisajili kwa wingi,” alifafanua Bi Chania.

Alisema viongozi wana jukumu la kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi ili kujisajili.

“Ninatoa wito kwa vijana kutoka eneo hili la Thika na Kaunti ya Kiambu kwa ujumla wajitokeza kwa wingi hasa kwa muda huu mchache wa mwezi mmoja,” akashauri.

You can share this post!

Wanamichezo bora Kenya mwaka 2021 kutuzwa katika kaunti ya...

TAHARIRI: Vijana wakatae hila, hadaa za wanasiasa