• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 2:55 PM
TAHARIRI: Vijana wakatae hila, hadaa za wanasiasa

TAHARIRI: Vijana wakatae hila, hadaa za wanasiasa

KITENGO CHA UHARIRI

UMESALIA karibu nusu mwaka hivi tuingie katika uchaguzi mkuu wa 2022, nalo joto la siasa linaendelea kusambaa kama moto katika kichaka kikavu.

Wanasiasa wanajipanga kuwamwagia vijana ‘sera zao tamu’, maneno ya mvuto na pesa za kuwashawishi kuwapigia kura.

Maazimio yao waliyoshindwa kuyatimiza na ile miradi bandia waliyowaanzishia vijana, wanarudi tena kuwalaghai ili wawape nafasi nyingine ya kuwatimizia malengo hayo.

Hii yote ni kero ya kura. Waliwashawishi vijana vivyo hivyo miaka mitano iliyopita, wakawaamini na kuwapa kura zao.

Walipopata uongozi wakawaona kinyaa. Wakawatoroka na kujificha wakiponda raha na familia zao.

Wakawatelekeza wale waliowapa vyeo.

Sera zile zile walizowaongopea mwanzoni, wakashindwa kuwatimizia matakwa yao, hivi wanarudi tena kuwahadaa kwazo.

Tunapaswa kutambua kwamba asilimia kubwa ya wapigakura nchini ni vijana. Mataifa mengi yakitaka kutekeleza ajenda zao kwanza lazima waulize, ‘kwani wao wanasemaje?’

Vijana hapa ndio wanaorejelewa kwani ndio nguvukazi ya jamii na nchi nzima kama vijana walengwa wakuu wa wanasiasa tuwe na msimamo thabiti dhidi yao.

Waliwaahidi ajira, hawakuziona. Wakaajiri wafanyakazi hewa na vitita vya pesa kujilimbikizia.

Hivi sasa mirengo mbali mbali ya kisiasa inaweka mikakati jinsi itakavyowatumia vijana ili kuwapenyeza kwenye debe.

Siku zote wanasiasa hawa huwashawishi vijana kufanya mambo fulani kama kuzua ghasia na rabsha kwa kuwaahidi malipo manono ama nafasi za ajira baadaye.

Lakini huwa ni uongo mtupu na wanawatumia vijana tu kwa maslahi yao kwa kuwa wana nguvu na ushawishi mkubwa katika jamii. Huu ndio wakati wa vijana kuungana na kupinga udhalimu huo unaofanywa na wanasiasa kila wakati wa kupiga kura.

Kura isiwatie tamaa ya kula. Wanasiasa nia yao ni kuwagonganisha vijana na kuwaharibia uhusiano mwema baina yao, wapigane na kusababisha vurugu nchini ilhali wanasiasa wapo kwenye makasri yao wanawatazama wakisagana na kuchinjana hovyo.

Ni wakati wa vijana kukengeuka na kupinga hadaa za wanasiasa. Ni jukumu la vijana kulilinda taifa lao dhidi ya wanasiasa madhalimu na wachochezi.

You can share this post!

Ni idadi ndogo tu ya wanaojitokeza Thika kujisajili wawe...

Raila kukita kambi ngome yake Ruto