Na GEOFFREY ANENE
SHEREHE za kutuza wanamichezo bora wa Kenya maarufu SOYA zitafanyika katika kaunti ya Kakamega mwezi Januari 2022.
Hii ni baada ya mwanzilishi wa tuzo hiyo Paul Tergat, ambaye ni rais wa Kamati ya Kitaifa ya Olimpiki Kenya (NOC-K) kusaini maelewano na Gavana wa Kaunti ya Kakamega Wycliffe Oparanya mnamo Oktoba 7.
Kakamega itakuwa kaunti ya nne kuandaa hafla hizo baada ya Nairobi, Mombasa na Nakuru.
Kauli mbiu ya hafla ya 2021 ni “Kutoka hali ya kujirekebisha hadi kupata nafuu tena.”
Washindi wa tuzo hiyo tangu ianzishwe mwaka 2005 ni Catherine Ndereba na Benjamin Limo (2005), Janeth Jepkosgei na Alex Kipchirchir (2006), muogeleaji Jason Dunford na Janeth Jepkosgei (2007), Samuel Wanjiru na Pamela Jelimo (2008) na mwanaraga Collins Injera na Linet Kirui (2009). Pia, kuna David Rudisha na Nancy Lagat (2010), Mary Keitany na David Rudisha (2012), Caleb Ndiku na Eunice Sum (2014) na mrushaji mkuki Julius Yego na Hyvin Kiyeng (2015), miongoni mwa wengine.
Washindi wa hivi punde wa tuzo hiyo ya kifahari ni nahodha mpya wa Harambee Stars Michael Olunga na mshindi mpya wa marathon kwenye Olimpiki Peres Jepchirchir. Walishinda makala ya 2020 yaliyofanyika mjini Naivasha katika kaunti ya Nakuru.