SHANGAZI AKUJIBU:
Nina miaka 38 na nimeamua kutafuta mume ili nitulie maishani. Hata hivyo, nina uhusiano wa pembeni na mume wa mtu. Penzi lake ni moto na sijui nitafanyaje nimuache nikatafute wangu.
Ni jambo la maana umegundua umuhimu wa kuwa na familia yako. Ingawa unafurahia penzi la mwanamume huyo, si wako na hatawahi kuwa wako. Jinsi pekee ya kutimiza nia yako ni kuvunja uhusiano huo uwe huru kutafuta wako.
Kuna tabia ya mpenzi wangu inanipa tumbojoto. Mara nyingi akipigiwa simu tukiwa pamoja huondoka kwenda kuzungumza kwa mbali.
Huyo ni mpenzi wako na hana sababu ya kukuficha chochote. Tabia yake ni ishara kwamba hataki ujue wanaompigia simu ama mazungumzo yao. Labda ana mpenzi mwingine na ndiye huwa anampigia. Chunguza mienendo yake kwa karibu ujue sababu.
Kuna mwanamume tunayefanya kazi pamoja ambaye anataka tuwe na uhusiano wa kimapenzi. Nampenda pia, lakini ninajua wanawake wengine huko kazini ambao wanammezea mate.
Msimamo wako huo unatokana na wivu. Kumbuka jamaa huyo amekuchagua wewe miongoni mwa wenzako. Hata kama wanamtaka, hawawezi kubadilisha uamuzi wake kwako.
Nina miaka 42 na nimeolewa. Juzi nilionja muwa nje kwa mara ya kwanza. Sijawahi kusikia muwa mtamu kama huo maishani. Mwenyewe yuko tayari kunipa wakati wowote nikitaka. Nafikiria kuacha ndoa. Waonaje?
Kipendacho roho ni dawa. Kama muwa unaozungumzia ndio muhimu kwako kuliko ndoa, raha jipe mwenyewe. Lakini je, una hakika gani kwamba mwenyewe atatimiza ahadi yake?