• Nairobi
  • Last Updated May 11th, 2024 5:59 PM
Obado ataka korti iamuru DPP kumpa taarifa ya mwanawe

Obado ataka korti iamuru DPP kumpa taarifa ya mwanawe

NA RICHARD MUNGUTI

ALIYEKUWA Gavana wa Migori Okoth Obado ameomba Mahakama Kuu iamuru Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) ampe taarifa ambayo mwanawe, Dan Aluoch, aliandika kuhusu mauaji ya mpenziwe Sharon Otieno mwaka 2018.

Imedaiwa Obado na mwanawe Dan walikuwa wanamchumbia Sharon, jambo ambalo gavana huyo wa zamani alisema “ni mwiko kwa mila ya Wajaluo mwana na baba kunywa maji kisima kimoja”.

Lakini Sharon alikanusha kabla ya kuuawa kwamba alikuwa amewafunga nira moja Obado na mwanawe Dan kimapenzi.

Mbali na taarifa hiyo ya mwanawe, pia Bw Obado aliomba Jaji Cecilia Githua aamuru afisi ya DPP impe taarifa zilizoandikwa na Bi Olivia Adhiambo, mlinzi wake Elvis Omondi, Hellen Adhiambo Odie na orodha ya simu za dereva wa teksi Jackson Otieno Gombe.

Jaji huyo alifahamishwa na mawakili Kioko Kilikumi, Rodgers Sagana na Prof Elisha Ongoya wanaowatetea Obado, Michael Oyamo na Casper Obiero wanaoshtakiwa kwa mauaji ya kinyama ya mwanafunzi wa chuo kikuu, Sharon Otieno, usiku wa Septemba 3, 2018.

Mahakama ilielezwa Obado na Obiero watategemea ushahidi huo wa Dan, Olivia, Hellen na dereva wa teksi Jackson Otieno Gombe kuwahoji mashahidi.

Licha ya kuitisha taarifa hizo, kiongozi wa mashtaka Bi Gikui Gichohi alisema: “DPP hatawaita watu hao taarifa zao zinaitishwa kama mashahidi katika kesi hiyo ya mauaji.”

Diwani wa zamani Lawrence Obonyo Mullah Owuor alieleza mahakama kwamba Sharon alikana alikuwa kwenye uhusiano wa kimapenzi na Dan Aluoch.

Alipotoa ushahidi, Mullah alisema alimpigia Sharon akiwa katika hoteli moja na Obado ndipo alikana walikuwa na uhusiano wa kimapenzi na Dan.

“Sharon alipiga picha mimba aliyokuwa nayo na kumtumia Dan huku akimweleza ‘aliye ndani ya tumbo ni ndugu yako, sitaki kuwa na uhusiano wowote nawe’,” Mullah  aliambia mahakama.

Pia aliongeza kusema Obado alimweleza ni mwiko katika mila ya Wajaluo baba na mwanawe kumchumbia msichana mmoja.

Olivia ni mkewe Obiero aliyemwajiri Gombe kazi ya kuendesha teksi yake (Olivia) na ambayo ilimsafirisha Sharon kuuawa ndani ya msitu Sondu.

Jaji Githua alielezwa Elvis Omondi ni afisa wa polisi aliyekuwa anamlinda Obado.

Gombe aliambia mahakama Elvis alimpigia simu kwenda hoteli ya Gracia kumchukua Sharon Otieno usiku ule aliuawa.

Jaji Githua alielezwa ni wajibu wa DPP kuwakabidhi washtakiwa taarifa yoyote itakayowasaidia kutendewa haki katika kesi inayowakabili.

Kesi inaendelea.

  • Tags

You can share this post!

Omanyala kuwania taji la Josko Laufmeeting dhidi ya...

Kocha Charles Okere kuongoza Vihiga Queens kwenye dimba la...

T L