Na Mohamed Ahmed
WABUNGE kutoka Pwani wametetea msimamo wao kukwamilia Chama cha ODM hata wakati ambapo wito umezidi kutolewa kuhusu uundaji chama maalumu cha Wapwani.
Mbunge Mwakilishi wa Wanawake Kaunti ya Kwale, Bi Zuleikha Hassan, amesema mpango wa kuunda chama Pwani hauna msingi kwa sasa.Badala yake, alisema mpango huo unakoroga wananchi pamoja na viongozi ambao wanatilia mkazo jambo hilo.
“Kwa sasa tumechelewa kabisa na pia kisheria hatupaswi kuwa na chama ambacho ni cha sehemu moja pekee. Hivyo basi ningewaomba viongozi wenzangu waache kutukoroga sisi wengine pamoja na wakazi wetu,” akasema Bi Hassan.
Alisema kuwa viongozi ambao wanataka Pwani ijitoe katika chama cha ODM wanapoteza wakati kwani chama hicho ndicho kinachowafaa Wapwani.Alisema ni kupitia kiongozi wa chama hicho cha ODM, Bw Raila Odinga, Pwani imeweza kufaidika kimaendeleo.
“Sisi kama Wapwani tulikuwa tunalilia ugatuzi na ni Bw Odinga alipigania nchi hii nzima kupata ugatuzi. Sisi tunafaa kusalia ndani ya ODM na tusikubali kuambiwa vingine,” akasema.
Mbunge wa Mvita, Bw Abdulswamad Nassir pia alisema kuwa Pwani haitatoka ODM na kuongeza kuwa viongozi wake wamechangia kukijenga na kukipa sifa chama hicho.
“Mimi binafsi na Gavana Hassan Joho pamoja na viongozi wengine tunasema kwa ujasiri kuwa tumechangia kuunda chama hiki. Hivyo basi sisi tuko ndani ya ODM mpaka mwisho,” akasema.
Bw Joho pia amesisitiza kuwa atapigania Urais kupitia chama hicho cha ODM.