MWANDISHI WETU
KINARA wa upinzani Raila Odinga alionyesha mapenzi yake kwa mkewe Ida Odinga katika siku ya kuzaliwa kwake Agosti 24th.
Wapenzi hao ambao pia walikuwa wakisherehekea miaka 50 kwenye ndoa, walijongewa na marafiki, wanasiasa, ndugu na jamaa katika hoteli ya kifahari ya Villa Rosa Kempinski, Nairobi.
Wanasiasa hao ni pamoja na Martha Karua, Kalonzo Musyoka, Eugene Wamalwa, na Babu Owino.
Mwanamuziki Akothee aka Esther Akoth, Prince Inda nao wakiwatumbuiza waalikwa.
Bw Odinga aliuasi ukapera mnamo Septemba 1, 1973. Alipokuwa akisomea katika Chuo Kikuu cha Nairobi (UON), Bi Ida alikutana na Bw Odinga ambaye alikuwa mfanyakazi katika kitengo cha Uhandisi wakati huo.
Akimmiminia sifa sufufu na kumtakia heri njema ya kuzaliwa kwake, Bw Odinga alimshukuru mkewe kwa kuwa nguzo ya familia yao.
“Kuwa kwenye ndoa kwa miongo tano kumeniletea furaha na kusherehekea kipindi hiki pamoja na siku ya kuzaliwa kwako ni jambo ninaloonea fahari. Mama Ida Odinga, tafadhali pokea shukrani zangu za dhati sio tu kwa kuwa mpenzi wangu bali mhimili wa maisha yangu na familia yetu,” akasema.
Bi Ida ambaye alisherehekea mwaka wake wa 73 wa kuzaliwa, alifanya kazi kama mwalimu kwa zaidi ya miaka 20 tangu alipohitimu masomo yake ya chuo kikuu.
Hata hivyo, baada ya mumewe kukamatwa mnamo 1982 na marehemu Rais Daniel Moi, Bi Ida aliendelea kuwalea watoto wao peke yake akifanya kazi ya ualimu.
Hata ingawa mumewe hajafanikiwa kuongoza nchi kama rais, Bi Ida amekuwa kigezo katika nchi kwa kushikilia nyadhifa mbalimbali.
Amewatetea kina mama, watoto na hata ubora wa afya nchini na kuwa mwanamke wa kwanza kuwa mkurugenzi mtendaji katika kampuni ya East African Spectre.
Wawili hao wamejaliwa na watoto wanne lakini mwana wao Fidel Odinga, aliaga dunia mnamo 2015.