• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:55 PM
Raila amsherehekea Mama Ida kwa mtindo katika hoteli ya kifahari

Raila amsherehekea Mama Ida kwa mtindo katika hoteli ya kifahari

MWANDISHI WETU

KINARA wa upinzani Raila Odinga alionyesha mapenzi yake kwa mkewe Ida Odinga katika siku ya kuzaliwa kwake Agosti 24th.

Wapenzi hao ambao pia walikuwa wakisherehekea miaka 50 kwenye ndoa, walijongewa na marafiki, wanasiasa, ndugu na jamaa katika hoteli ya kifahari ya Villa Rosa Kempinski, Nairobi.

Wanasiasa hao ni pamoja na Martha Karua, Kalonzo Musyoka, Eugene Wamalwa, na Babu Owino.

Mwanamuziki Akothee aka Esther Akoth, Prince Inda nao wakiwatumbuiza waalikwa.

Bw Odinga aliuasi ukapera mnamo Septemba 1, 1973. Alipokuwa akisomea katika Chuo Kikuu cha Nairobi (UON), Bi Ida alikutana na Bw Odinga ambaye alikuwa mfanyakazi katika kitengo cha Uhandisi wakati huo.

Akimmiminia sifa sufufu na kumtakia heri njema ya kuzaliwa kwake, Bw Odinga alimshukuru mkewe kwa kuwa nguzo ya familia yao.

 

Kinara wa Azimio Raila Odinga na mkewe Ida wakati wa hafla ya kusherehekea miaka 50 ya ndoa yao katika hoteli ya Villa Rosa Kempinski, Nairobi, Agosti 24, 2023. Picha|Hisani

“Kuwa kwenye ndoa kwa miongo tano kumeniletea furaha na kusherehekea kipindi hiki pamoja na siku ya kuzaliwa kwako ni jambo ninaloonea fahari. Mama Ida Odinga, tafadhali pokea shukrani zangu za dhati sio tu kwa kuwa mpenzi wangu bali mhimili wa maisha yangu na familia yetu,” akasema.

Bi Ida ambaye alisherehekea mwaka wake wa 73 wa kuzaliwa, alifanya kazi kama mwalimu kwa zaidi ya miaka 20 tangu alipohitimu masomo yake ya chuo kikuu.

Hata hivyo, baada ya mumewe kukamatwa mnamo 1982 na marehemu Rais Daniel Moi, Bi Ida aliendelea kuwalea watoto wao peke yake akifanya kazi ya ualimu.

Hata ingawa mumewe hajafanikiwa kuongoza nchi kama rais, Bi Ida amekuwa kigezo katika nchi kwa kushikilia nyadhifa mbalimbali.

Amewatetea kina mama, watoto na hata ubora wa afya nchini na kuwa mwanamke wa kwanza kuwa mkurugenzi mtendaji katika kampuni ya East African Spectre.

Wawili hao wamejaliwa na watoto wanne lakini mwana wao Fidel Odinga, aliaga dunia mnamo 2015.

 

  • Tags

You can share this post!

Chomelea ashtakiwa kwa kumpachika tineja mimba

Mbunge aliyeumizwa na wahuni afika DCI kwa kitimaguru

T L