• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 6:39 PM
Ronaldo afikia rekodi ya ufungaji bora wa mabao kimataifa

Ronaldo afikia rekodi ya ufungaji bora wa mabao kimataifa

Na MASHIRIKA

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

CRISTIANO Ronaldo alifunga penalti mbili katika sare ya 2-2 iliyosajiliwa na timu yake ya taifa ya Ureno dhidi ya Ufaransa katika mchuano wa mwisho wa Kundi F kwenye Euro.

Ufanisi huo wa Ronaldo, 36, ulimwezesha kufikia rekodi ya mabao 109 ambayo imekuwa ikishikiliwa na Ali Daei wa Iran kati ya mwaka 1993 na 2006. Daei na Ronaldo ndio wanasoka wa pekee wa kiume kuwahi kufunga zaidi ya mabao 90 wakivalia jezi za nchi zao kwenye mapambano ya kimataifa.

Ni tukio ambalo kwa sasa linatarajiwa kumpigisha Ronaldo hatua zaidi kwenye mijadala kuhusu nani mchezaji bora wa muda wote duniani.Kufikia sasa, Ronaldo tayari ndiye mshikilizi wa rekodi ya mfungaji bora wa muda wote katika soka ya ngazi ya klabu. Aidha, ameibuka mfungaji bora katika soka ya bara Ulaya mara tano sasa.

Dhidi ya Ufaransa, Ronaldo aliweka rekodi ya kuwa mfungaji bora katika Kombe la Dunia pamoja na Euro, hivyo kumpiku aliyekuwa fowadi matata wa Ujerumani, Miroslav Klose aliyekuwa akijivunia magoli 19. Ronaldo aliweka rekodi ya kuwa mfungaji bora wa Euro mnamo Juni 15 wakati ambapo Ureno walikuwa wakicheza na Hungary. Mabao yake kwa sasa kwenye kipute hicho ni 13.

Takriban nusu ya mabao ya Ronaldo yamefungwa katika kipindi cha dakika 30 za mwisho wa mechi. Kufikia sasa, amepachika wavuni magoli 31 katika dakika 15 za mwisho na 22 kati ya dakika 61 na 75 ya mchezo.Ronaldo amefunga mabao 17 kati ya dakika 16-30 na mara 16 kati ya dakika 31-45.

Mabao yake 11 yametokea chini ya dakika 15 za mwanzo wa mechi huku 12 yakifumwa wavuni chini ya dakika 15 za mwanzo wa kipindi cha pili.Amefunga mabao 89 akiwa ndani ya kijisanduku na 20 mengine akiwa nje ya kijisanduku cha wapinzani.

Kati magoli hayo, 14 yametokana na mikwaju ya penalti na tisa mengine yamekuwa zao la mipira ya ikabu au frikiki.Lithuania na Uswidi ndizo timu ambazo Ronaldo amezifunga mara nyingi zaidi (mabao saba). Hadi kufikia Jumatano usiku katika jiji la Budapest nchini Hungary, hakuwa amefunga bao lolote dhidi ya Ufaransa.

Wanasoka wanaofuata sasa Ronaldo na Daei ni Mokhtar Dahari aliyechezea Malaysia katika miaka ya 70 na 80 na akafunga mabao 89. Wengine ni Ferenc Puskas aliyefungia Hungary mabao 84 kutokana na mechi 85 pamoja na na Godfrey Chitalu aliyefungia Zambia magoli 79 kati ya 1960 na 1980.

Christine Sinclair wa Canada ndiye anashikilia rekodi ya dunia ya ufungaji bora katika soka ya wanawake baada ya kufunga mabao 186 kutokana na mechi 299.Ronaldo aliyewaongoza Ureno kutwaa taji la Euro 2016 nchini Ufaransa sasa amempiku Lionel Messi ambaye kwa sasa ni sehemu ya kikosi cha Argentina kwenye Copa America.

Mabao 109 ambayo Ronaldo amefungia Ureno katika mechi 178 ni rekodi bora ikilinganishwa na magoli 73 ambayo Messi amefungia Argentina kutokana na michuano 147. Ina maana kwamba Messi ambaye kwa sasa ana umri wa miaka 33, anahitaji miaka 27 mingine ili kufikia rekodi ya mabao 100. Kwa kuwa hayo ndiyo magoli amefunga kuanzia 2015, ina maana kwamba atahitaji miaka saba zaidi ili kufikia rekodi ya Ronaldo ya magoli 109.

Mabao ya Ronaldo

31 – Mechi za kufuzu kwa Euro

31 – Mechi za kufuzu kwa Kombe la Dunia

19 – Mechi za kirafiki kimataifa

13 – Mechi za Euro

7 – Mechi za Kombe la Dunia

5 – Mechi za Uefa Nations League

2 – Mechi za Kombe la Mashirikisho

  • Tags

You can share this post!

Uhispania kumenyana na Croatia katika 16-bora baada ya...

Wazazi walee watoto wao ipasavyo kwani ni amana kutoka kwa...