• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 1:01 PM
Safari ya mwisho ya Ayimba yaanza na misa ya wafu South B

Safari ya mwisho ya Ayimba yaanza na misa ya wafu South B

Na AYUMBA AYODI

TAFSIRI: GEOFFREY ANENE

Rafiki na familia ya kocha wa zamani wa timu ya Kenya Shujaa, marehemu Benjamin Ayimba hapo Juni 8, walisherehekea maisha yake katika kanisa la Katoliki ya Our Lady Queen of Peace mtaani South B, Nairobi.

Mkewe Ayimba, Caroline Waswa na mke wake wa zamani Lois Onyango na watoto wao Brian, Gabriel, Keenan na Eli walihudhuria misa ya wafu, ingawa mwili wa Ayimba haukuwepo.

Hata hivyo, rafiki wataweza kutazama mwili wake na kutoa heshima zao za mwisho hapo Juni 9 ugani RFUEA kwenye barabara ya Ngong Road kuanzia saa sita adhuhuri.Ayimba atazikwa Ijumaa katika katandogo ya Uranga katika kaunti ya Siaya.

Wengine waliofika katika misa hiyo ni mwenyekiti wa Shirikisho la Raga Kenya (KRU) Oduor Gangla na msemaji wa familia ya Ayimba, Oscar Osir, ambao walikuwa watu pekee walioruhusiwa kutoa hotuba kanisani ya kuomboleza mwendazake Ayimba.

Osir alikuwa meneja wa timu wakati Ayimba alikuwa kocha wa Shujaa ilipofika nusu-fainali ya Kombe la Dunia la raga ya wachezaji saba kila upande kwa mara ya kwanza kabisa mwaka 2009.

Wengine waliotoa rambirambi zao nje ya misa hiyo ni mwenyekiti wa zamani wa KRU, Mwangi Muthee, mwenyekiti wa Shirikisho la Ligi ya Raga Kenya (KRLF) Edward Nyakwaka na nahodha wa timu ya Shujaa mwaka 2009 Humphrey Kayange.

Gangla alisema Ayimba alikuwa kama ndugu yake, mchezaji nyota wa raga, kiongozi wa wanaume, supastaa wa dunia na rahisi wa kusema ukweli bila ya kujali unauma. “Benja alipenda watoto wake, maisha na Mungu,” alisema Gangla. “Picha yake akiwa amepiga magoti kushukuru Mungu baada ya Kenya kuingia Olimpiki mwaka 2016 bado iko akilini mwetu na mioyoni mwetu.”

Osir alisema Ayimba, 44, alipenda kila mtu na kila kitu alichogusa, lakini hakuwa wa kuyumbayumba wakati wa kufanya maamuzi bila kuyabadilisha.

Muthee alisema Ayimba alikuwa balozi mkubwa wa mchezo wa raga. “Tunazungumzia sifa zake, ari, ushirikiano…alikuwa na vitu hivyo vyote ambavyo vinahusiana na raga,” alisema Muthee, akisema kuwa mchezo wa raga ulichukua nguvu zake zote baada ya kujituma kabisa uwanjani. “Aliaga dunia akiwa amevalia buti zake za raga miguuni,” alisema Muthee.

Kayange alisema kuwa Ayimba alimsaidia sana katika ukuaji wake wa raga mwaka 2006 alipomteua kuwa nahodha akipuuza wachezaji wengine wazoefu kikosini.

“Nilipokutana naye kwa mara ya kwanza mapema 2006, alinipuzilia mbali akisema mimi ni mwembamba, na siwezi kustahimili mchezo wa raga. Alisema nahitaji kuwa na misuli zaidi,” alisema Kayange ambaye alishangaa kuona Ayimba akimteua kuwa nahodha mwisho wa mwaka 2006.

  • Tags

You can share this post!

Vitengo vinne vikuu kuwakabili polisi watendao maovu

Wamaasai waonya Tangatanga dhidi ya kujaribu kupenya Narok