• Nairobi
  • Last Updated May 11th, 2024 5:59 PM
Tanzia: Mwanafunzi mwenye ulemavu akiteketezwa na moto Kaiyaba hadi kufa

Tanzia: Mwanafunzi mwenye ulemavu akiteketezwa na moto Kaiyaba hadi kufa

Na SAMMY KIMATU

MWANAFUNZI mwenye ulemavu alifariki Jumatatu, Julai 24, 2023 kufuatia kisa cha moto uliozuka eneo la Mandazi Road, katika mtaa wa mabanda Mukuru-Kayaba, Nairobi.  

Akithibitisha kisa hicho, Kamanda wa polisi eneo la Makadara, Bi Judith Nyongesa alisema George Muriu mwenye umri wa miaka 15 aliaga dunia baada ya moto kuteketeza nyumba yao.

Aliongeza kuwa kanisa, stoo ya viatu makaa na nyumba nne ziliteketea katika kisa hicho cha Jumatatu asubuhi.

Kulingana na babake marehemu, Dominic George Muriu Muga, moto huo ulisababishwa na mtu aliyewasha gurudumu nyuma ya kanisa linalopakana na mto Ngong.

“Nimempoteza mwanangu wa pekee. Awali alihusika katika ajali ya barabarani baada ya kugongwa na pikipiki. Ajali hiyo ilimsababishia ulemavu kichwani, mikononi na miguuni. Hata hivyo, hilo halikumzuia kuenda shuleni,” Bw Muga alisema.

Alikuwa mwanafunzi wa darasa la saba kafika Shule ya Msingi ya St Catherine’s, South B

Mwanamume akionyesha kitandani ambapo mvulana wa Gredi ya 7 alifariki baada ya kisa cha moto katika eneo la Mandazi Road, Mukuru-Kaiyaba, Kaunti Ndogo ya Starehe. Mkuu wa polisi eneo la Makadara, Bi Judith Nyongesa alisema maafisa wa polisi wameanzisha uchunguzi kuhusu tukio hilo. Picha|SAMMY KIMATU

Aidha, babake aliambia vyombo vya habari kwamba alifiwa na mkewe miaka miwili iliyopita na ameachwa na watoto watatu wasichana.

Katika eneo la tukio, moshi ulikuwa ukipofuka mvunguni mwa kitanda ambapo marehemu alikutana na maafa.

Taifa Leo Dijitali ilipomzuru, nguo kadhaa za wateja wake zilionekana kuungua Mzee Muga akifichua alichuma riziki kwa kufulia watu nguo.

Bw Dominc Muthwii, shahidi-mwathiriwa alisema moto huo ulianza dakika chache kabla saa kumi na mbili za asubuhi lakini ulikuwa mkubwa na kuchochewa na upepo.

Kulingana naye, ulikuwa mkubwa kiasi cha kutoweza kuuzima.

“Ni jambo la kusikitisha wahuni walitumia jukwaa la moto kuiba mabati yaliyosalia,” Muthwii alishangaa.

Miundomsingi ya barabara eneo hilo ni mbovu, kiasi kuwa gari la kuzima moto lisingeweza kuingia.

Majirani wakimfariji mzee Dominic George Muga baada ya kifo cha mwanawe wa Gredi ya 7 baada ya kisa cha moto katika eneo la Mandazi Road, katika mtaa wa mabanda wa Mukuru-Kaiyaba, Starehe. Picha|SAMMY KIMATU

Hata hivyo, wenyeji walijikakamua kupambana na moto wakitumia maji kutoka mto Ngong na hatimaye kufanikiwa kuuzima.

Kulingana na mkuu wa tarafa eneo hilo, Bw Solomon Muranguri, hakuna majeruhi waliripotiwa.

“Nawapongeza vijana wa Kaiyaba kwa kujituma kudhibiti kuenea kwa ndimi za moto ndiposa nyumba nyingi hazikuathirika,” Bw Muranguri akasema.

Kanisa la New Israel, pia liliathirika kutokana na moto huo.

Kamanda wa polisi Makadara, Bi Judith Nyongesa aliarifu kuwa uchunguzi umeanzishwa kubaini kiini cha mkasa huo.

 [email protected]

  • Tags

You can share this post!

Mahakama yaizima serikali kumpokonya Jomo silaha

Shakahola: Awamu ya nne upasuaji maiti yaanza

T L