Na KELVIN KAGAMBO, ripota Mwananchi Communications Limited
Katika kitabu chake cha The End of Jobs, milionea kijana Taylor Pearson ameandika, “kwa enzi hizi za matumizi makubwa ya mashine na intaneti, ajira yako ni kitu kinachoweza kupotea kufumba na kufumbua, kwa hiyo ujasiriamali ni salama zaidi ya ajira.”
Nasema katika enzi hizi za matumizi makubwa ya mashine na intaneti na siasa chafu za Afrika, hakuna uthabiti wowote katika ajira wala ujasiriamali.
Kama unavyoweza kuamka ukaambiwa kampuni iliyokuajiri inapunguza wafanyakazi, ndivyo unavyoweza kuambiwa Serikali imepiga marufuku uuzwaji wa nguo za mitumba, wakati huo wewe una shehena ya mashati ya mitumbo huko stoo.
Ninachojaribu kukwambia ni kwamba, siku yoyote unaweza kuwa huna chanzo cha kupata pesa tena.
Na mwamamume bila pesa ni mwanamume dume suruali. Na hili sio mpaka uambiwe, hapana! Litaanzia kwako mwenyewe, taratibu utaanza kujiona unapoteza ‘hamu’ ya kuwa mwanamume.
Sasa kila mwanamume anajua cha kufanya asipokuwa na kazi, ni kimoja tu, kutafuta kazi nyingine, lakini wengi hatujui nini hatutakiwi kufanya tusipokuwa na kazi, na leo ndiyo tutazungumzia hicho.
Hufanyi hivi ili majirani wasijue kibarua kimeota nyasi, hapana. Unafanya hivi ili nyumbani wasikuzoee, kwa sababu kwa mazoea tu, unaweza kushangaa mkeo anakutuma ukalete mwiko, na ukiona umeshafika huku, jua pointi inayofuata inakuhusu.
Mkeo akisema, “Baba Brian, naomba muangalie mtoto mara moja niende dukani.” Wewe utasikia kasema, “Baba Brian, kwa sababu huna hela na huna kazi, umekaa hapa siku nzima unapoteza muda kwa kuangalia TV utadhani unalipwa, sasa kaa na mtoto, mimi naenda dukani kununua cha kupika hapa, ili nipike, ule, ujaze hilo tumbo, upate nguvu ya kushika rimoti na kuendelea kubadilisha chaneli, na kupoteza muda zaidi.”
Kuanzia hapo utamjibu vibaya, atakujibu vibaya pia, mtajibizana, matokeo yake hakuna hata kitakachopikika kabisa.
Kwa hiyo ili usifikie huku, ni vyema sana kujitahidi kutokuwa na mtazamo hasi kuhusu mkeo.
Yaani, usiwe na mtazamo hasi kiasi kwamba hata akisema jambo baya kukuhusu, wewe lichukulie kwa upesi.