Na GEORGE ODIWUOR
MZOZO wa kisiasa unatokota katika chama cha ODM baada ya viongozi wa chama hicho kutofautiana kuhusu kutimuliwa kwa mwenyekiti wa eneo bunge la Karachuonyo, Bw George Maigo.
Huku baadhi ya wajumbe wakiunga mkono kuondolewa kwa afisa wa eneo hilo, wapo wanaopinga mchakato huo na kumtaka aendelee kuhudumu.
Bw Maigo aliondolewa afisini na kundi la wajumbe na nafasi yake kuchukuliwa na Timothy Adede wakati wa mkutano uliofanyika Kendu Bay wiki jana.
Alishutumiwa kwa uongozi mbaya, jambo ambalo linadaiwa kufanya chama tawala, UDA kupata nguvu katika Kaunti ya Homa Bay.
Aidha, viongozi kutoka kaunti hiyo wanasemekana kuhusika na kutimuliwa kwake.
Wamemshutumu mwenyekiti huyo kwa kukosa kufanya mikutano ya kujadili njia za kuimarisha ODM.
Hata hivyo, katibu wa chama katika kaunti hiyo, Bw Ong’ondo Were na mbunge wa Karachuonyo, Bw Adipo Okuome walisema kutimuliwa kwa mwanasiasa huyo sio hatua nzuri kwa ODM na kwamba mchakato huo haukufuata utaratibu ufaao.
Bw Were alisema wanachama wa ODM wanapaswa kukumbatiana na afisa kubadilishwa iwapo tu amefariki.
“Kubadilishwa kunaweza pia kutokea ikiwa afisa ataamua kuhamia chama kingine,” alisema.
Aliwataka wanachama kukumbatia maridhiano na kukumbatia wanasiasa waliojitokeza kuwa wagombeaji huru baada ya kujiondoa ODM.
Bw Okuome alisema mabadiliko ya uongozi wa chama yaliyofanywa katika eneo bunge lake huenda yakasababisha mzozo ndani ya ODM kabla ya wengine kuchukua fursa ya mizozo hiyo kuwatatiza zaidi.