NA SHABAN MAKOKHA
VIONGOZI wa Kanisa Katoliki Kaunti ya Kakamega wakiongozwa na Askofu Joseph Obanyi, wametofautiana na wanasiasa kuhusu kufungwa kwa shule ya Upili ya Wasichana ya Sacred Heart Mukumu.
Shule hiyo ilifungwa kwa muda usiojulikana, baada ya wanafunzi 124 kulazwa katika hospitali ya Rufaa ya Kakamega baada ya kuathiriwa na chakula na maji, shuleni humo.
Wasimamizi wa shule hiyo walithibitisha wanafunzi wawili, mmoja kutoka Kaunti ya Bungoma na mwingine kutoka eneo la Navakholo, Kaunti ya Kakamega, walikufa kutokana na maradhi yaliyochangiwa na chakula au maji ambayo si salama.
Wanafunzi wengine zaidi ya 500 pia waliathirika.
Awali, wanafunzi 124 walilazwa hospitalini wakihara ,kutapika na kuhisi kizunguzungu.
Pia idadi ya wanafunzi waliolalamika kuhisi uchovu iliendelea kuongezeka.
Askofu aliwalaumu Seneta Boni Khalwale na Mbunge Mwakilishi wa Kike, Bi Elsie Muhanda katika kaunti hiyo, kwa kuchochea kufungwa kwa shule hiyo baada ya maradhi hayo kulipuka.
Shule hiyo ilifungwa na afisa wa Elimu, Bw Jared Opiyo kwa muda usiojulikana mnamo Aprili 3, 2023.
Dkt Khalwale na Bi Muhanda waliandamana na afisa huyo wa elimu wakati wa kufungwa kwa shule hiyo.
Subscribe our newsletter to stay updated