Na AFP
SAN JUAN, UFILIPINO
WAUMINI sugu wa Kanisa Katoliki ‘wamesulubishwa’ kwenye misalaba ya mbao huku wengine wakicharazwa mijeledi migongoni kuonyesha mateso aliyopitia Yesu Kristo siku ya Ijumaa Kuu nchini Ufilipino.
Japo watu wengi katika nchi hiyo, yenye idadi kubwa ya Wakatoliki waliadhimisha siku hiyo kushiriki ibada au kujumuika na familia zao, wengine walitubu dhambi zao na kutafuta baraka za Mungu.
Katika kijiji cha San Juan, kaskazini mwa Manila, mamia ya wakazi na watalii walitazama kwa mshangao maigizo ya matukio wakati wa kusulubiwa kwa Yesu Kristo.
Wanaume wengi waliovalia mataji yaliyotengenezwa kwa mmea wa zabibu, walitembea bila viatu katika barabara nyembamba wakicharazana kila mara kwa mijeledi.
Damu ilitiririka migongoni mwao na kulowesha long’i zao huku wakishabikiwa na makundi ya watu waliokongamana nje ya maduka na nyumba zao za makazi.
Baadhi ya waumini hao walisimama kisha kujilaza ardhini ili wacharazwe na wenzao kwa mijeledi na vipande vya mbao.
Damu ilipokoma kutoka kwenye vidonda vyao, miili yao ilikwaruzwa kwa nyembe au nyundo yenye vipande vya glasi ili itokwe na damu zaidi.
“Huwa nafanya hivi ili familia yangu iwe na afya nzuri,” akasema Daren Pascual, 31, baada ya kucharaza mgongo wake kwa mjeledi kujiandaa kwa shughuli kamili. Unahitaji kuomba, kisha hautahisi uchungu,” akasema.
Katika hatua ya mwisho ya maigizo hayo, wanaume watatu, wakisindikizwa na mtu aliyevalia kama kamanda wa jeshi la Warumi, walielekezwa kwenye rundo la takataka ambapo wawili kati yao walifungwa kwenye misalaba ya mbao.
Wilfredo Salvador, mvuvi wa zamani, ambaye aliigiza nafasi ya Yesu Kristo, alihiari mikono ya miguu yake kupigwa misumari, kwenye msalaba, huku droni zikipaa angani na watalii wapiga picha kwa simu zao.
Baada ya dakika kadha, misumari iling’olewa na Salvador akateremshwa ardhini.Alibebwa kwa machela na kupelekwa ndani ya hema iliyotundikwa kando ili kufanyiwa ukaguzi- kabla ya kuelekea nyumbani kwa teksi yenye magurudumu matatu.
“Mungu hutupa nguvu za kimwili tofauti na wengine ambao hawawezi kustahimili uchungu,” akasema Salvador, 66, ambaye alianza kushiriki maigizo ya kusulubishwa, miaka 15 iliyopita baada ya kupatwa na matatizo ya kiakili.
“Mimi hufanya hivi kwa kujitolea. Nashukuru Mungu kwa kunipa maisha ya pili,” akasema.
Maigizo hayo yamekuwa yakifanywa katika vijiji vilivyoko viungani mwa jiji la San Fernando kwa miongo kadha iliyopita.
Lakini shughuli hizo zilipigwa marufuku miaka mitatu iliyopita kutokana na janga la Covid-19.
Idara ya afya imeonya washiriki wa maigizo ya Pasaka kuhusu hatari ya wao kuambukizwa ugonjwa wa pepopunda na maradhi mengine.
“Ni wazi kwamba kusulubiwa kwa Kristo kunalenga kuokoa walimwengu kutoka kwa dhambi,” akasema Padri Jerome Secillano, Katibu wa kamati kuhusu masuala ya umma katika Muungano wa Maaskofu Wakatoliki Ufilipino.
“Ukitaka kusamehewa dhambi, nenda ukatubu,” akaongeza.
Subscribe our newsletter to stay updated