• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 7:50 PM
Wamiliki wa shule zilizolemewa na makali ya Covid-19 wageuza madarasa kuwa vyumba vya biashara

Wamiliki wa shule zilizolemewa na makali ya Covid-19 wageuza madarasa kuwa vyumba vya biashara

Na SAMMY WAWERU

MADARASA ya shule za wamiliki binafsi nchini zilizolemewa na makali ya Covid-19 kiasi kwamba zimeshindwa kuafikia masharti ya serikali wakati huu ambapo masomo ya shuleni yamerejelewa baada ya zaidi ya miezi tisa, yamegeuzwa kuwa vyumba vya biashara.

Shule kote nchini zimefunguliwa leo Jumatatu, Januari 4, 2021 miezi tisa baada ya kufungwa kufuatia mkurupuko wa virusi vya corona.

Kwenye uchunguzi wa Taifa Leo, tayari shule zilizoathirika zimeweka vibango vya matangazo ya kukodisha madarasa kuwa maduka na ofisi, huku uga ukigeuzwa bustani.

Shule ya mmiliki binafsi ya Kastemil iliyoko eneo la Kasarani, Thika Road na Brain Stone Academy, Githurai, zimegeuza madarasa yake kuwa vyumba vya biashara.

“Mwishoni mwa 2020 tuliarifiwa tuendee chochote tunachomiliki shuleni kwa sababu haitafunguliwa tena,” Caroline Ng’ang’a mmoja wa walimu Brain Stone Academy akaambia Taifa Leo.

Sawa na shule hizo, wazazi wa Grand Kago Academy, Karatina mwaka uliopita, 2020, walitakiwa kuanza kutafutia wanao shule zingine, mmiliki akiwaarifu gharama kuafikia sheria na mikakati ya ufunguzi kudhibiti maenezi ya virusi vya corona shuleni imemlemea.

Maelfu ya watoto waliokuwa katika shule za kibinafsi zilizoathirika huenda wakafungiwa nje, kutokana na idadi kubwa ya wanafunzi wanaotarajiwa kujiunga na shule za umma.

Kulingana na chama cha shule za wamiliki binafsi nchini (KPSA), watoto wapatao 56,000 wameathirika hasa baada ya shule walikokuwa wakisomea kufungwa kwa sababu ya wamiliki kushindwa kuafikia mahitaji ya ufunguzi.

Kila shule imetakiwa kuhakikisha imeweka mikakati na mipangilio maalum kuzuia wanafunzi kuambukizwa Covid-19 shuleni.

You can share this post!

Wilson Bii aduwaza Samwel Muchai

Southampton yaipokeza Liverpool kichapo cha 1-0