NA BRIAN OCHARO
WATU wawili wameshtaki wa kwa kuingia kwa njia haramu kwenye meli ya mizigo iliyokuwa inabeba miti ya mbuyu kwenda Georgia.
Ali Mbaraka na Hassan Ali walifikishwa mbele ya mahakama ya Mombasa jana kwa tuhuma za kushindwa kuripoti kuondoka kwao wakiwa kwenye meli hiyo kwa afisa wa uhamiaji aliye karibu.
Mashtaka yanaonyesha wawili hao walipatikana wakiwa wamejificha ndani ya MV RIVER MAS mlikokuwa miti hadi walipogunduliwa siku mbili kabla ya meli hiyo kuondoka kutoka bandari ya Mombasa.
Washukiwa hao pia walifunguliwa mashtaka kwa kosa la kuingia katika meli hiyo bila idhini.
Washukiwa hao walikiri makosa hayo walipofikishwa mbele ya Hakimu wa Mombasa Vincent Adet.
Waliiomba mahakama kuwaonea huruma wakisema familia zao zinawategemea.
Serikali ilisema washukiwa walitenda makosa hayo Agosti 24, katika Bandari ya Mombasa.
Washukiwa wamezuiliwa rumande wakisubiri hukumu.