• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 7:50 PM
Wazazi wa wanafunzi wanaoteketeza mabweni walipe gharama – Serikali

Wazazi wa wanafunzi wanaoteketeza mabweni walipe gharama – Serikali

DAVID MUCHUNGUH na CHARLES WASONGA

WAZAZI sasa watalazimika kulipia gharama ya ukarabati wa shule zilizoharibiwa na watoto wao huku majengo zaidi ya shule yakiteketezwa Jumatano katika wimbi la utovu wa nidhamu miongoni mwa wanafunzi nchini.

Waziri wa Elimu George Magoha Jumatano alikariri msimamo wa serikali kwamba wanafunzi wanatakaopatikana na hatia ya kuhusika katika vitendo hivyo vya uhalifu watakamatwa na kushtakiwa.

“Mtoto yeyote ambaye ana umri wa zaidi ya miaka minane ataweza kushtakiwa. Tunashirikiana na idara ya upelelezi wa jinai kufanikisha hili. Uovu huu sharti ukome. Kwa hivyo, jengo lolote lililoteketezwa litajengwa upya na wazazi,” akasema.

Miongoni mwa shule ambazo majengo yao yameteketezwa wiki hii ni Shule ya Upili ya Wavulana na Moi Nyatike ambako bweni lilichomwa na wanafunzi, Shule ya Upili ya Kigama, iliyoko kaunti ya Vihiga na Shule ya Upili ya Wavulana ya Karumandi iliyoko kaunti ya Kirinyaga ambako pia mabweni yaliteketezwa.

Wanafunzi watano wamekamatwa kuhusiana na visa hivyo.

Profesa Magoha amewaamuru wakurugezi wa elimu kuitisha mikutano ya bodi za elimu katika kaunti kufikia Februari 25, 2021 kwa lengo la kupendekeza njia za kukomesha fujo shuleni.

“Wizara imetoa taarifa kuhusu usalama katika shule za upili za mabweni, ambayo itaongoza bodi simamizi za shule katika kuweka mikakati ya kuzuia kutokea kwa visa kama hivyo shuleni,” Profesa Magoha akasema.

Alikuwa wakiongea na wanahabari alipozuru Shule ya Msingi ya Kwa Njenga katika kaunti ndogo ya Embakasi Kusini, kaunti ya Nairobi.

Awali, Profesa Magoha amewalaumu wazazi kwa kufeli kuwapa nidhamu watoto, na hivyo kuchangia ongezeko la visa vya utovu wa nidhamu shuleni.

Wiki jana alikosolewa kufuatia pendekeza lake kwamba adhabu ya kiboko inaposa kurejeshwa shuleni. Adhabu hiyo ilipigwa marafuku mnamo mwaka wa 2001, sheria Watoto ilipofanyiwa marekebisho.

Profesa Magoha aliongeza kuwa visa vya utovu wa nidhamu pia vinasababishwa na matumizi ya dawa za kulevya miongoni mwa wanafunzi, uovu ambao alisema umekithiri nyumbani.

Chama cha Kitaifa cha Walimu Nchini (Knut) na kile cha kutetea masilahi ya walimu wa shule za upili (Kuppet), vikisema vitawagonganisha walimu na wanafunzi.

You can share this post!

Mamelodi Sundowns yatinga 16-bora Nedbank Cup bila Mkenya...

Mvua ya mabao Old Trafford