NA KALUME KAZUNGU
BARABARA ambayo ni kiunganishi cha pekee kufikia vijiji vya Salama, Juhudi, Widho, Marafa, Mashogoni na viungani mwake imetajwa kuwa ni ya kuibua kumbukumbu za mauaji na vilio.
Vijiji hivyo tangu vianzishwe miaka karibu 10 iliyopita vimeshuhudia changamoto ya Al-Shabaab, wanakijiji wakiishia kuuawa kinyama ambapo miili yote inayokusanywa na polisi hupitia barabara hii.
Ni hali ambayo imesukuma wanavijiji kuichukia.
Wengi wanadai barabara hiyo inaandamwa na mkosi na husafirisha maiti kwa wingi.
Isitoshe, magaidi wa Al-Shabaab pia wamekuwa wakiteka nyara wanavijiji, ambapo huwatembeza kilomita kadhaa kwenye barabara hiyo kabla ya kuwachinja.
Mzee wa umri wa miaka 50, George Summit, ambaye alikuwa bawabub wa shule ya msingi ya Majembeni mnamo Septemba 20, 2023, alikamatwa na kundi la Al-Shabaab na kutembezwa kutoka Majembeni hadi kijiji chao cha Widho-Mashambani ambapo wapiganaji hao walimuua kwa kumchinja shingoni.