• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 12:48 PM
Kindiki atakiwa kutuliza uhalifu Pokot Magharibi

Kindiki atakiwa kutuliza uhalifu Pokot Magharibi

NA OSCAR KAKAI

KAMATI ya usalama katika bunge la kitaifa itamuita tena Waziri wa Usalama wa Ndani Kithure Kindiki kujibu maswali kuhusu hali ya usalama katika eneo la Kaskazini mwa Bonde la Ufa.

Kamati hiyo inazuru Kaunti za Pokot Magharibi na Elgeyo Marakwet kutathimini hali ya usalama katika eneo lenye utata la Bonde la Kerio.

Jumamosi, Desemeba 9, 2023 kamati hiyo ilipokea mapendedekezo kutoka kwa wakazi wa maeneo hatari ya Chesegon na Turkwel kuhusu hali ya utovu wa usalama katika eneo hilo ambapo kaimu mwenyekiti wa kamati hiyo Dido Rasso alimsuta Prof Kindiki kwa kupeana askari wa akiba katika kaunti za Turkana, Elgeyo Marakwet, Samburu na kuacha kaunti ya Pokot Magharibi.

Dido pia ni mbunge wa Saku.

“Kwa nini hakuipa Pokot Magharibi askari wa akiba?” akashangaa mbunge huyo.

Kamati hiyo, hata hivyo, iliipongeza wizara ya usalama wa ndani ikisema kuwa maafisa wanaofanya oparesheni wamefaulu kuleta utulivu katika baadhi ya maeneo kaunti za Samburu na Turkana ambapo visa vingi vya utovu wa usalama vimepungua.

Kuhusu elimu, kamati hiyo masomo kuwa itawaagiza Prof Kindiki na mwenzake wa Elimu Ezekiel Machogu kuhakikisha kuwa taasisi zote za usalama zinafanya kazi ili kuimarisha masomo katika eneo hilo.

Bw Dido aliwahakikishia wakazi kuwa shule zote ambazo zilifungwa kutokana na utovu wa usalama katika eneo hilo zinafunguliwa.

“Tutahakikisha kuwa usalama unaimarishwa shuleni,” alisema.

Alisema kuwa suala la mpaka lazima lisuluhishwe.

Viongozi wa kaunti hiyo waliokuwa wameandamana na kamati ya usalama bungeni ni Gavana wa Pokot Magharibi Simon Kachapin, naibu wake, Robert Komolle na wabunge; Peter Lochakapong (Sigor) na Samuel Moroto (Kapeguria), miongoni mwa wengine.

Kachapin kwa upande wake alisambaza msaada wa chakula cha msaada kwa wakazi ambao wameathirika na utovu wa usalama, akiahidi msaada zaidi wa kaunti.

Gavana huyo vilevile alililia serikali ya kitaifa kusaidia maeneo yaliyoathirika na utovu wa usalama kwa misaada mbalimbali ya kimsingi.

Bw Lochakapong alisema kuwa shule 5 katika eneo la Chesegon bado zimefungwa kutokana na suala la wizi wa mifugo.

Naye Bw Moroto alisuta maafisa wa usalama wanaohudumu katika eneo hilo, akilalamikia kwamba wamezembea kazini.

 

 

  • Tags

You can share this post!

Avokado ni dhahabu shambani mwake  

Hayawi hayawi…Jackie Matubia afichua mchumba wake mpya  

T L