NA WINNIE ONAYNDO
GAVANA wa Nairobi, Johnson Sakaja Alhamisi, Desemba 14, 2023 alizindua rasmi Kituo cha kutoa Huduma kwa Wateja kilichoboreshwa.
Kituo hicho kinajivunia teknolojia ya kisasa, ikijumuisha kituo ambacho akina mama wanaweza kuwahudumia na hata kuwayonyesha watoto wao.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Gavana Sakaja aliangazia maendeleo ambayo serikali yake imefanya tangu aingie madarakani.
Alitaja mpango wa lishe shuleni, ambao unatarajiwa kuanza kutoa huduma kwa watoto 190, 000 kuanzia Januari 2023, uzinduzi wa ICU ya kwanza katika Hospitali ya Rufaa ya Mama Lucy Kibaki, ufufuaji wa Uwanja wa Dandora, miongoni mwa miradi mingine katika azma yake ya kuboresha Kaunti ya Nairobi.
“Kaunti itaendesha mafunzo ya kina kwa wale watakaohusika ili kuwezesha utoaji wa huduma bora kwa wateja. Ninatoa wito kwa timu inayosimamia Huduma kwa Wateja kujipanga ipasavyo ili kuhakikisha wafanyikazi wote wamesajiliwa na kupewa kadi ili waweze kutimiza majukumu yao kwa ufanisi,” akasema Gavana Sakaja.