WATAALAMU wa afya wamewataka Wakenya kuwa waangalifu baada ya kugunduliwa kwa aina mpya ya magonjwa ya zinaa nchini.
Magonjwa hayo yana uhusiano wa karibu na kisonono (gonorrhea) na wataalamu wa Taasisi ya Utafiti wa Matibabu nchini (KEMRI) wanasema kuwa hayajawahi kuonekana humu nchini awali.
Naibu mtafiti mkuu katika Kituo cha Utafiti kuhusu Viini katika KEMRI, Profesa Samson Muuo, alifichua kugundua kuwa wanawake wote 424 Wakenya wenye umri wa kuanzia miaka 15 kwenda juu walioshiriki utafiti huo uliofanywa katika hospitali mbili walionyesha dalili za maradhi ya kisonono na chlamydia.
Alieleza Taifa Leo kuwa wahusika walilalamika kuhusu kuwashwa, uchungu na kuvimba kwenye sehemu nyeti, harufu mbaya, kutoka uchafu, kuwashwa wakati wa haja ndogo, kuvuja damu kwa njia isiyo ya kawaida na uchungu kwenye sehemu ya chini ya mgongo.
“Habari hizi zilikusanywa kutoka kwa wanajamii katika sehemu moja na bado zinachunguzwa hivyo basi tutajua hivi karibuni ni wangapi walitumia kinga, historia yao ya kutumia dawa za kuua viini kwa sababu wengi wao waliashiria kuwa wamezitumia hapo awali, maambukizi mengineyo na iwapo wamewahi kupata maradhi kama hayo hapo awali. Hatukufanya vipimo vya HIV kwa sababu havikuwa sehemu ya lengo la utafiti.”
Watafitiwa walikuwa wanawake wanaoshiriki ngono na waliotimia umri wa uzazi zaidi ya miaka 15 na pia walikubali kushiriki utafiti kwa hiari.
“Aina mbili ya jeni tulizogundua kwa jina MtrR na 23S rRNA zinazohusishwa na hali ya kukataa tiba, hazina uhusiano na aina ya maradhi yaliyoripotiwa awali. Busia ambao ni mji wa mpakani unatoa mwelekeo bora kuhusu kusambaa kwa ugonjwa huo. Inaweza ikachukuliwa kuwa maambukizi haya yatasambaa kati ya maeneo haya mawili,” alisema Profesa Muuo.
“Katika utafiti huu, chembechembe zilitwaliwa kutoka sehemu nyeti za wanawake walioonesha dalili za maradhi hayo ya zinaa. Aina tatu ya maradhi ya zinaa ikiwemo aina mpya ya kisonono, Chlamydia na Mycoplasma ziligunduliwa katika wanawake hao wote 424 walioteuliwa kushiriki utafiti huo.”
Akizungumza na Taifa Leo kwa njia ya simu, mtaalam wa maambukizi katika Afisi ya Kimaeneo katika Shirika la Afya Duniani (WHO-AFRO) Shillah Simiyu, alisema Busia ina idadi kubwa ya maradhi ya zinaa kutokana na kiwango cha juu cha shughuli za ngono kutokana na kwamba ni mji wa mpakani ambapo madereva hupumzika wanapokuwa safarini.