NA ALEX KALAMA
ALIYEKUWA Waziri wa Utalii katika serikali ya utawala wa Jubilee Bw Najib Balala amefikishwa katika Mahakama Kuu ya mji wa Malindi akisubiri kujua hatima yake kuhusu kesi ya ufisadi inayomkabili ya ubadhirifu wa fedha za umma takriban Sh8.5 bilioni za ujenzi wa chuo cha utalii cha Ronald Ngala kilichoko eneo la Vipingo katika Kaunti ya Kilifi.
Bw Balala na aliyekuwa Katibu wa wizara Leah Adda Gwiyo pamoja na Joseph Odero, wanakabiliwa na mashtaka 10 ikiwemo ufujaji wa fedha hizo zilitolewa katika hazina ya Tourism Fund kwa minajili ya ujenzi wa chuo hicho.
Bw Odero ni mhandisi wa West Consult Engineers.
Msemaji wa Tume ya Maadili na Kukabiliana na Ufisadi (EACC) Bw Eric Ngumbi alisema Bw Balala alikamatwa jijini Nairobi na ambapo baadaye akasafirishwa kwa ndege hadi Mombasa kabla ya kupelekwa katika mahakama ya Malindi kukabiliwa na mashtaka.
“Wamekamatwa baada ya Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP) kuidhinisha mashtaka,” amesema Bw Ngumbi.