• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 1:14 PM
Ezra Chiloba ajiuzulu kutoka wadhifa wake wa Mkurugenzi Mkuu wa CA baada ya kukabiliwa na tuhuma za ufisadi

Ezra Chiloba ajiuzulu kutoka wadhifa wake wa Mkurugenzi Mkuu wa CA baada ya kukabiliwa na tuhuma za ufisadi

NA LABAAN SHABAAN

MKURUGENZI Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Kenya (CA) Ezra Chiloba ambaye amekuwa akimulikwa kwa tuhuma za ufisadi na usimamizi mbaya, amejiuzulu.

Taarifa iliyotolewa na CA mnamo Oktoba 19, 2023, na ikatumwa kwa vyombo vya habari imesema Bw Chiloba aliandikia Mwenyekiti wa Bodi ya mamlaka hiyo Mary Mungai kumwarifu kwamba amejiuzulu.

“Kwa niaba ya CA, ninamtakia Mkurugenzi Mkuu anayeondoka ufanisi katika siku za usoni na kushukuru mchango wake muhimu sana kwa shirika hili na sekta pana ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano,” Bi Mungai amesema, akithibitisha wamekubali kujiuzulu kwake.

Bw Chiloba alisimamishwa kazi kwa muda mwezi Septemba 2023, lakini akakana tuhuma alizoelekezewa za kuhusika katika sakata ya kifedha katika asasi hiyo na usimamizi mbaya.

Bw Chiloba alitaja tuhuma hizo zilizoko katika ripoti ya ukaguzi wa usimamizi wa fedha katika CA kama madai tu.

“Haya ni madai tu. Nitasubiri mkondo wa haki ufuatwe ili ukweli kuhusu suala hili ujulikane,” alinukuliwa kwenye mahojiano mafupi saa chache baada ya bodi ya tume hiyo kumsimamisha kazi kwa wakati usiojulikana.

Bw Chiloba alisimamishwa kazi baada ya mkutano wa bodi ya CA ulioongozwa na mwenyekiti wake, Bi Wambui.

“Baada ya mkutano wa bodi ya Mamlaka hii uliofanyika Septemba 18, 2023, na kupendekeza kusimamishwa kazi kwa mkurugenzi mkuu, ni furaha yangu kujulisha wafanyakazi kuhusu uteuzi wa Christopher Wambua kuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu kuanzia leo (Jumatatu, Septemba 18, 2023,” hadi wakati usiojulikana,” akasema Bi Wambui kwenye taarifa.

Kulingana na ripoti ya ukaguzi, Chiloba alijipendelea kwa kutuma maombi na kuidhinisha mkopo wake wa nyumba kwa kiwango cha juu kwa thuluthi mbili.

Aidha, afisa huyo anadaiwa kujihusisha na mgongano wa kimasilahi kwa kujitwika wajibu wa kuwa mnunuzi na muuzaji katika biashara ambapo CA ililipa Sh25 milioni.

Bw Chiloba pia alilaumiwa kwa mienendo mibaya na ukiukaji wa maadili baada ya kubainika kuwa alinunua nyumba na shamba la ukubwa wa ekari saba badala ya shamba la ekari moja inavyohitajika na mpango wa watumishi wa umma kuhusu ununuzi wa nyumba.

“Vile vile, mkurugenzi huyo mkuu aliwasamehe wafanyakazi waliogura CA wakiwa na mkopo wa kima cha Sh28.9 milioni na akapunguza masalio ya mikopo ya wafanyakazi wa zamani,” ikasema ripoti hiyo ya ukaguzi.

Ripoti hiyo pia ilifichua sakata ya usimamizi mbaya wa mpango wa mkopo wa nyumba katika mamlaka ya CA, ambao umetoa mkopo wa zaidi ya Sh662 milioni kwa wafanyakazi wa sasa na wale wa zamani.

Inapendekeza hatua za kinadhamu zichukuliwe dhidi ya Bw Chiloba na maafisa wengine watano wa ngazi za juu katika mamlaka hiyo.

Maafisa hao ni pamoja na wakurugenzi wa idara za huduma za wafanyakazi, huduma za kisheria, huduma za kifedha na mkaguzi wa ndani.

Ukaguzi huo, ambao uliendeshwa na idara za ukaguzi za CA na Hazina ya Kitaifa, uliamriwa na bodi ya mamlaka hiyo mnamo Mei 2023.

Imefichua kuhusu jinsi wafanyakazi wa sasa na wa zamani wa mamlaka hiyo walivyotumia vibaya mpango huo wa mkopo wa nyumba.

Uovu huo, haswa uliendeshwa kupitia matumizi ya wataalamu wa kibinafsi wa kukadiria thamani ya mali kama nyumba na ardhi waliotoa thamani ya juu.

Kuhusiana na tuhuma za Bw Chiloba, ilibainika kuwa wakadiriaji hao wa kibinafsi waliweka thamani ya nyumba na ardhi ambayo afisa huyo alinunua kuwa Sh25 milioni.

Hii ni licha ya kwamba wakadiriaji wa serikali waliweka thamani ya mali hizo kuwa Sh16.72.

Ripoti hiyo ya ukaguzi inasema kuwa Bw Chiloba aliomba na kuidhinisha mkopo wa nyumba kumwezesha yeye kununua mali hiyo kutoka kwa Simiyu Wakhungu.

Oktoba 2021, Bw Chiloba aliteuliwa kuwa Mkurugenzi Mkuu wa CA na amehudumu kwa miaka miwili kabla ya kubwaga zana za kazi Oktoba 18, 2023.

  • Tags

You can share this post!

Kaburi la bahati nzuri lavutia watalii kutoka pembe zote za...

Familia 100 zapiga hesabu upya baada ya kuhamishwa pahala...

T L