Na RICHARD MUNGUTI
ALIYEKUWA mbunge wa Laikipia Kaskazini Bw Mathew Lempurkel alishtakiwa upya Januari 13, 2022 kwa matamshi ya uchochezi.
Bw Lempurkel aliyewakilishwa na Bw Saitabai ole Kanchory alikana shtaka la kuchochea hisia za chuki dhidi ya watu wenye mashamba makubwa katika kaunti ya Laikipia.
Bw Lempurkel anadaiwa alitoa matamshi hayo wakati wa mahojiano na kituo cha televisheni cha Maa TV mnamo Julai 17, 2021.
Shtaka hilo lilidai matamshi hayo yalilenga kuibua hisia za chuki dhidi ya wamiliki wa mashamba makubwa.
Bw Lempurkel alikana shtaka hilo mbele ya hakimu mwandamizi katika mahakama ya Milimani Bw Bernard Ochoi.
Bw Kanchory aliomba mahakama iamuru dhamana aliyopewa mshtakiwa mwaka 2021 imgharimie mshtakiwa sasa.
Bw Ochoi aliamuru dhamana aliyolipa mshtakiwa mwaka 2021 imsimamie.
Kesi hiyo itatajwa tena Februari 16, 2022 kwa maagizo zaidi.