• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 3:13 PM
Mwanamume ashtakiwa kwa kulaghai muuzaji wa dawa ya sumu ya nyoka

Mwanamume ashtakiwa kwa kulaghai muuzaji wa dawa ya sumu ya nyoka

NA RICHARD MUNGUTI

MWANAMUME ameshtakiwa kwa kumlaghai mfanyabiashara kitita cha Sh1.7 milioni akidai ameshinda zabuni ya kuuza dawa za kutibu sumu ya nyoka nchini Sudan Kusini.

Nicholas Ndunda Kilungya aliyefikishwa mbele ya hakimu mkuu katika mahakama ya Milimani Lucas Onyina alijifanya daktari mwenye tajriba ya juu alipomlaghai Bw Felix Munyao Kikanga Sh1,731,800.

Onyina alifahamishwa Kilungya alitumia ujanja kumlaghai Bw Kikanga.

“Unakabiliwa na shtaka la kumlaghai Bw Kikanga Sh1,731,800 ukidai ulikuwa umeshinda zabuni ya kupeleka nchini Sudan Kusini kuuza dawa ya kutibu makali ya sumu ya nyoka. Ni ukweli au sio ukweli?” Bw Onyina alimuuliza mshtakiwa.

“Sio ukweli,” Kilungya alijibu.

Kilungya alikabiliwa na shtaka la kula njama za kumlaghai Bw Kikanga katika kaunti ya Nairobi kati ya Feburuari 5 na Machi 1 2023.

Kiongozi wa mashtaka Anderson Gikunda alieleza mahakama kuwa mshtakiwa anayetoka Kaunti ya Machakos alijua bayana hakuwa na zabuni ya kuuza dawa hizo za tiba ya sumu ya nyoka Sudan Kusini.

Mahakama ilielezwa eneo hilo la Sudan Kusini liko na nyoka wenye sumu kali mithili ya wale waliowakabili wana wa Israel katika jangwa la Sinai walipokuwa wakielekea Canaan wakitoka utumwani Misri miaka ya kale.

Onyina alifahamishwa Kilungya alijitwalia pesa hizo kwa kujifanya alikuwa ameshinda zabuni hiyo ya kupelekea nchi hiyo dawa za kutibu wanaoumwa na nyoka.

Kilungya aliomba aachiliwe kwa dhamana akisema hatatoroka ila atuhudhuria vikao vyote vya kusikilizwa kwa kesi hiyo.

Kiongozi wa mashtaka Anderson Gikunda hakupinga ombi hilo la dhamana.

Onyina alimwamuru mshtakiwa alipe dhamana ya pesa taslimu Sh200,000.

Mahakama ilimwamuru Gikunda amkabidhi mshtakiwa nakala za mashahidi ajue namna ya kujitetea.

Kesi itatajwa baada ya wiki mbili.

  • Tags

You can share this post!

Rubis yawaweka sawa madereva Safari Rally ikianza

Atwoli avuna matunda ya uaminifu kwa Ruto

T L