• Nairobi
  • Last Updated May 13th, 2024 9:17 PM
Sherehe zatuliza vita vya ubabe Kirinyaga

Sherehe zatuliza vita vya ubabe Kirinyaga

KENNEDY KIMANTHI na GEORGE MUNENE

SAWA na kaunti nyingine, Kaunti ya Kirinyaga inayoandaa sherehe za Mashujaa Dei mwaka huu 2021, imekumbwa na uhasama wa kisiasa wa kila mara, kushukiana na migogoro ya kila mara baina ya viongozi.

Hata kwa waangalizi wasio makini, dalili za ubabe wa kisiasa katika kaunti hiyo huwa wazi.

Katika miaka ya sabini, kulikuwa na tofauti za kisiasa kati ya wanasiasa wakuu wa Kirinyaga James Njiru (Kanu Moto) na Nahashon Njuno, waliokuwa wabunge wa Ndia na Gichugu mtawalia.

Wawili hao wanakumbukwa kwa kurushiana mangumi Bungeni wakati Njiru alikuwa akihudumu kama waziri msaidizi wa Afya huku Njuno akiwa waziri msaidizi wa wizara ya Uchukuzi na Mawasilino.

Pia, wanakumbukwa kwa kutishiana kwa bunduki mjini Kutus baada ya kutofautiana kuhusu mahali ambapo makao makuu ya Kanu yangejengwa.

Ingawa wawili hao waliacha siasa kitambo, ushindani mkali wa kisiasa ungali unashuhudiwa kaunti ya Kirinyaga.

Japo uhasama wa kisiasa Kirinyaga sio jambo geni, sherehe za Mashujaa Dei zinaonekana kutuliza hali na kuunganisha viongozi wa kaunti hiyo kwa wakati huu.

Wanakubaliana kwamba, kuna haja ya kuzika tofauti zao na kuhakikisha kaunti yao inapata maendeleo na ustawi. Ni azimio ambalo Rais Uhuru Kenyatta alisisitiza Jumatatu alipokutana na viongozi wa Kirinyaga katika ikulu ndogo ya Sagana kabla ya sherehe za leo Jumatano ambazo ni za kitaifa na zinazofanyika katika kaunti hiyo.

Rais Kenyatta aliwataka viongozi hao kuungana na kushirikiana kama kundi moja ili kuafikia maendeleo na ustawi was kaunti yao.

Kirinyaga ina maeneobunge manne Kirinyaga Ndia, Kirinyaga Central, Gichugu na Mwea ambayo kila moja limewahi kuwa mzozo wa viongozi.

Sherehe za Mashujaa Dei mwaka huu 2021 zitafanyika katika uwanja wa michezo wa Wang’uru dunia ikiendelea kupambana na janga la Covid-19.

Katibu wa usalama wa ndani, Karanja Kibicho na Gavana wa Kirinyaga Anne Waiguru walisema walipatana kwa ajili ya kufanikisha sherehe hizo ambazo zimefanya kaunti hiyo kupata miradi kadhaa ya miundomsingi.

You can share this post!

Hofu ya siasa za urithi kutawala Mashujaa Dei

Waiguru amtaka rais azungumzie mrithi wake

T L