Na KIPKOECH CHEPKWONY
GAVANA wa Kirinyaga Ann Waiguru anaamini serikali itatimiza Ajenda Kuu Nne za maendeleo kabla ya kukamilika kwa hatamu ya Rais Uhuru Kenyatta.
Akihutubu kwenye uwanja wa Wang’uru wakati wa Sikukuu ya Mashujaa, Bi Waiguru alisema katika miaka minne iliyopita, kaunti zimepiga hatua kubwa kuhusu miradi hiyo.
“Nataka nieleze kwa ufupi yale mashujaa wa Kirinyaga wameweza kutimiza katika miaka minne. Katika kutimiza Ajenda Kuu Nne, tumewasaidia wakulima kuongeza uzalishaji chakula. Ujenzi wa zaidi ya nyumba 100 mjini Kerugoya unakaribia kukamilika. Tunajenga hospitali yenye vitanda 342. Haya ni mambo yanayotekelezwa kwingine pia,” akasema Bi Waiguru.
Alipozindua Ajenda Kuu Nne, Rais Uhuru Kenyatta alilenga kuwepo Chakula cha Kutosha, Huduma za Afya kwa Wote, Ustawishaji Viwanda na Nyumba za Bei Nafuu.
Gavana Waiguru alisema wafanyabiashara sasa wanafanya kazi katika mazingira bora, baada ya kujengewa masoko ya kisasa 15.