• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 4:42 PM
Taharuki kuhusu teknolojia ya kutambulisha nyuso

Taharuki kuhusu teknolojia ya kutambulisha nyuso

NA MARY WANGARI

DELHI, India

TEKNOLOJIA ya vifaa vya kutambulisha nyuso katika shule kadhaa zinazofadhiliwa na serikali nchini India imezua hofu kuhusu ukiukaji wa haki za usiri wa data.

Wanaharakati wa kutetea haki za kibinadamu kidijitali wametaja teknolojia hiyo kama “ukiukaji uliovuka mipaka” kutoka kwa serikali na kuingilia faragha ya watoto.

Hatua hiyo ya kuanzisha teknolojia ya kutambulisha uso imefuatia uamuzi wa serikali ya jiji la Delhi 2019, wa kupachika kamera za CCTV katika shule zaidi ya 700 ili kuhakikisha usalama wa wanafunzi.

“Mifumo hiyo ya kutambulisha sura inawekwa pasipo sheria za kudhibiti ukusanyaji na matumizi ya data, jambo ambalo ni la kuhofisha hasa kwa watoto,”

“CCTV tayari ni ukiukaji wa haki za watoto kuhusu faragha, hata ingawa baadhi ya wazazi walikuwa wameiunga mkono kwa usalama wa watoto wao…lakini matumizi ya teknolojia ya kutambulisha uso ni ukiukaji uliokithiri na si haki kamwe,” alifafanua Anushka Jain, wakili katika Wakfu wa Uhuru kuhusu Intaneti, kundi la wanaharakati lililofahamu kuhusu uzinduzi huo wiki iliyotangulia.

Jain alieleza vyombo vya habari kuwa matumizi ya teknolojia hiyo kwa watoto ina matatizo kwa sababu uhakiki wake ni wa kiwango cha chini mno, hivyo basi, endapo ni katika kisa cha uhalifu, watoto wanaweza kutambulishwa visivyo.

“Ingekuwa vigumu kwa wazazi kufahamu kuhusu hatari zinazohusiana na ukiukaji na matumizi mabaya ya sheria kuhusu uhifadhi wa data,” alisema.

Teknolojia ya kutambulisha sura inatumika pakubwa katika viwanja vya ndege, vituo vya treni na mikahawa kote nchini India.

Kuna mipango ya kuanzisha mfumo wa kitaifa wa kufanyia mageuzi ya kisasa kikosi cha polisi ikiwemo michakato yake ya kukusanya vitambulisho vya wahalifu.

Wachanganuzi hata hivyo, wanasema manufaa yake hayajabainishwa wazi, na kwamba itakiuka haki za watu kuhusu faragha.

Wamehoji kuwa itasababisha udadisi zaidi wenye vidhibiti vichache na ufafanuzi finyu kuhusu jinsi teknolojia hiyo inavyofanya kazi, jinsi data inavyohifadhiwa na ni nani anaweza kuipata.

You can share this post!

Waliomuua msichana 9, wakimtoa mapepo wakamatwa

Wanahabari wataka waorodheshwe kwa watakaopewa chanjo ya...