• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 5:55 AM
Viongozi kukongamana kwa mkutano wa UNGA

Viongozi kukongamana kwa mkutano wa UNGA

Na AFP

NEW YORK, Amerika

VIONGOZI wa ulimwengu wiki hii watakongamana katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa (UN) jijini New York, kwa Kikao cha 76 cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UNGA).

Kwa mara ya kwanza tangu mlipuko wa janga la Covid-19 mwaka 2020, viongozi hao wanafanya mkutano wa ana kwa ana kinyume na 2020 ambako walituma taarifa zao kupitia video.

Hata hivyo, thuluthi moja ya mataifa 193 bado yatatuma video kwa mkutano huo.Miongoni mwa mada kuu zitakazojadiliwa katika mkutano huo, ni juhudi mpya za kupambana na athari za Covid-19 na Mabadiliko ya Tabianchi.

Hatua ambazo ulimwengu umepiga katika utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDG) pia zitaajdiliwa katika kikao hicho cha UNGA ambacho pia kitahudhuriwa na wakuu wa mashirika ya kimaendeleo ya kimataifa.

Rais wa Amerika Joe Biden atahutubia kikao hicho kesho Jumanne, kwa mara ya kwanza tangu alipoingia mamlakani mnamo Januari 20, 2020.

Balozi wake katika UN Linda Thomas-Greenfield, alisema Biden “atazungumzia masuala yenye umuhimu mkubwa kwetu: kutokomezwa kwa Covid-19, kupambana na mabadiliko ya tabia nchi, kutetea haki za kibinadamu, demokrasia na uthabiti ulimwenguni.”

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Jumamosi aliondoka kuelekea Amerika kuhudhuria mkutano huo ambapo anatarajiwa kuhutubia kikao hicho Alhamisi wiki hii.

Hii ndio itakuwa ziara ya kiongozi huyo nje ya bara Afrika tangu alipoingia mamlakani Machi 19, 2021 kufuatia kifo cha Rais John Pombe Magufuli.

Mara ya mwisho Rais wa Tanzania kuhutubia mkutano wa UNGA ilikuwa mnamo 2015 na alikuwa Rais wa awamu ya nne wa taifa hilo, Jakaya Mrisho Kikwete.

Amerika imesema kuwa kila kiongozi atakayeingia katika ukumbi mkuu wa mkutano sharti athibitishe kuwa amepewa chanjo dhidi ya Covid-19.

Utawala wa jiji la New York pia umeweka kituo cha muda nje ya lango kuu la Makao Makuu ya UN ambako kuna wahudumu wa kuwapa wageni chanjo aina ya Johnson & Johnson, bila malipo.

Chanjo hii hutolewa mara moja.

Katibu Mkuu wa UN Antonio Guterres , aliwaambia wanahabari kwamba umoja huo unalenga kuhakikisha kuwa asilimia 70 ya watu ulimwenguni watakuwa wamepewa chanjo kufikia Juni, 2022.

Alisema kufikia sasa jumla ya dozi 5.7 bilioni za aina mbalimbali ya chanjo zimetolewa kote ulimwenguni.

Bara la Afrika limepokea asilimia mbili pekee ya dozi hizo.

You can share this post!

Wakenya wamiminika UG kununua mafuta

Amani: Kalonzo kutuzwa leo Dubai