• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 7:50 AM
FAUSTINE NGILA: Vita vya Iran, Israel visizuie ukuaji wa teknolojia nchini

FAUSTINE NGILA: Vita vya Iran, Israel visizuie ukuaji wa teknolojia nchini

Balozi wa Iran nchini Jafar Barmaki Iran (kushoto), makamu wa rais wa nchi hiyo Sorena Sattari (kati) na waziri wa Habari na Teknolojia nchini Joe Mucheru, wakikata utepe wakati wa uzinduzi wa kituo cha uvumbuzi na teknolojia (Iran House of Innovation and Technology-IHIT) katika eneo la Kilimani, Nairobi wiki iliyopita. Picha/Evans Habil

Na FAUSTINE NGILA

Juhudi za hivi majuzi za taifa la Iran za kuinua viwango vya ubunifu, teknolojia na biashara baina yake na Kenya zimeonekana kuikera Israeli, mataifa hayo mawili yakiwa na uhasama mkuu katika eneo la Mashariki ya Kati.

Iran wiki hii, inazindua kituo cha uvumbuzi na teknolojia kwa jina The Iran House of Innovation and Technology (IHIT), ambacho kinalenga kutoa nafasi ya biashara na intaneti bila malipo kwa kampuni za Kenya na Iran.

Akitaja mpango huo kama mkubwa zaidi duniani ulioanzishwa na Terhan, balozi wa Iran humu nchini Jafar Barmaki alisema kampuni 40 kutoka taifa lake zitahudhuria kuzinduliwa kwa kituo hicho.

Licha ya kuwa Kenya ni taifa linalohitaji usaidizi wa kiteknolojia katika kila pembe, Israeli imetaja mpango huo kama suala la kiusalama, hasa ikizingatiwa mataifa hayo mawili yamekuwa yakikomoana kiteknolojia huku kila moja likijaribu kudukua mitandao ya mwenzake kwa uhabirifu mkubwa.

“Iran inaendelea kuzua misukosuko ya kiusalama eneo la Mashariki ya Kati na Afrika kwa kufadhili mitandao ya kigaidi na kusambaza teknolojia na silaha kwa mataifa mbalimbali,” Israeli ilisema kwenye Facebook ilipogundua mpango wa Iran nchini Kenya.

Ingawa mataifa yote yanapendezwa na hali ya teknolojia nchini, huenda uhasama baina yao ukaathiri mipango ya kusaidia nchi hii kupiga hatua kiteknolojia, na kusambaratisha diplomasia ambayo umekuwepo baina ya Israeli Kenya.

Kituo hicho kitakuwa eneo la Milimani, Nairobi, ambapo ni karibu na makao ya ubalozi wa Israeli nchini, na kuna hatari ya mataifa haya kutumia Kenya kama uwanja wa vita vya kiteknolojia, ambapo Wakenya ndio wataumia zaidi.

Kimsingi, Kenya iko mbali mno kufikia upeo wa teknolojia wa Israeli na Iran, na serikali yetu isipoingilia kati na kutuliza joto hili la kidiplomasia, huenda raia wakaumia sana mataifa haya yakianza vita vya ubabe wa kiteknolojia nchini.

Serikali, kupitia wizara za Teknohama na Mambo ya Kigeni, inafaa kuwa mbioni kuchunguza madai ya Israeli, na kuwaambia Wakenya kwa nini Yerusalemu inahisi kuwa kutakuwa na utovu wa usalama mitandaoni Iran ikiruhusiwa kuzindua kituo cha teknolojia Nairobi.

Ni wazi kuwa Israeli imekuwa na maadui wengi katika Mashariki ya Kati, kama vile Iran, Iraq, Lebanon, Oman, Qatar, Kuwait na Syria na hata Afrika (Somalia, Libya, Algeria, Tunisia, Mali, Niger, Djibouti na Mauritania), lakini ilikuwa taifa la kwanza nchini Kenya kujenga ofisi za ubalozi, kabla ya kujinyakulia uhuru.

Ili kulinda wananchi dhidi ya athari ya vita hivi, si busara kwa serikali kuendelea kutekeleza mpango wa Iran bila kuzingatia masuala yaliyoibuliwa na Israeli, kwani farakano litokeapo, sisi nyasi ndio tutaumia – mitandao yetu itadukuliwa, bila kusahau mtandao mzima wa umeme nchini.

Serikali ichukulie suala hili kwa uzito. Hakuna haja ya taifa lenye uwezo mkubwa wa teknolojia kama Kenya kuzimiwa ndoto yake na mataifa yaliyopiga hatua kubwa tayari kwenye ulingo huo wa teknohama.

You can share this post!

Mvua ya mabao Old Trafford

CHARLES WASONGA: Serikali ikome kuhujumu vyama vya kutetea...