• Nairobi
  • Last Updated May 21st, 2024 10:36 AM
Watu 20 waangamia katika mlipuko wa tangi la mafuta Lebanon

Watu 20 waangamia katika mlipuko wa tangi la mafuta Lebanon

Na MASHIRIKA

ALTALIL, Lebanon

WATU 20 waliuawa na wengine 79 wakajeruhiwa katika mlipuko wa tangi ya mafuta katika eneo la Akkar, kaskazini mwa Lebanon, Shirika la Msalaba Mwekundu nchini Lebanon lilisema Jumapili kupitia Twitter.

Taifa hilo linakabiliwa na changamoto kubwa la uhaba wa mafuta hali inayochangia foleni ndefu kushuhudiwa katika katika vituo vya kununua bidhaa hiyo na gesi. Vile vile maeneo kadha yameshuhudia giza kutokana na ukosefu.

Duru za kijeshi na polisi zilisema kuwa wanajeshi wa Lebanon walikuwa wamenasa tangi moja ya kuhifadhi mafuta katika mji wa Altalil. Walipokuwa wakijaribu kuwapa raia mafuta hayo ndipo mlipuko huo ukatokea.

Walioshuhudia tukio hilo walisema karibu watu 200 walikuwa karibu na eneo ambako mlipuko huo ulitokea.

Hata hivyo, kulitokea maelezo ya kukinzana kuhusu chanzo cha mlipuko huo.

“Watu walikuwa wanakimbia na mabishano kati ya baadhi yao walichangia mmoja wao kufyatua risasi. Risasi hiyo iligonga tangi ya mafuta na ikalipuko,” afisa mmoja wa usalama ambaye aliomba asitajwe alisema.

Aliongeza kuwa miongoni mwa waliofariki na kujeruhiwa na wanajeshi na maafisa wengine wa usalama.

Runinga ya Al-Jadeed TV nayo iliripoti kwa moto huo ulianzishwa na mtu aliyewasha kiberiti karibu na tangi hiyo ya mafuta.

Abdelrahman, ambaye aliteketea usoni na mwilini na ambaye alilazwa katika hospitali ya al-Salam mjini Tripoli, ni mmoja wa wale ambao walikuwa wamepanga foleni kununua mafuta.

Mashahidi wengine waliambia shirika la habari la Reuters kwamba wakazi wa Akkar, wenye ghadhabu, waliokuwa wamekusanyika katika eneo la tukio ndio waliwasha moto huo ambao pia tuliteketeza malori mawili ya mafuta.

Tafsiri: CHARLES WASONGA

You can share this post!

Wanasiasa watoroka mazishi ya Chidzuga kwa kuzuiwa kupiga...

Jagina wa soka kambini mwa Bayern na Ujerumani, Gerd Muller...