• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:08 PM
Nafasi finyu mjini lakini ufugaji mbuzi umenawiri si haba

Nafasi finyu mjini lakini ufugaji mbuzi umenawiri si haba

Na SAMMY WAWERU

KEVIN Uduny amekuwa akifuga mbuzi kwa muda wa miaka minane, na hana nia ya kuacha shughuli hiyo asilani.

Yeye ni mwasisi wa shamba linalojulikana kama Toggfarm, lililoko katika eneo la Huruma, Nairobi.

“Nilianza kufanya shughuli hii kwa kuwafuga mbuzi wawili niliowanunua kutoka Kiamaiko kwa Sh3,000 kila mmoja,” asema Uduny. Mnamo mwaka 2014, yeye, pamoja na wenzake, waliomba ufadhili kutoka kwa serikali kupitia kwa mpango wa ‘Njaa Marufuku’ ambapo walipata ufadhili wa Sh150,000.

“Pia, tulipata mafunzo,” aongeza mkulima huyo.

“Tuliwanunua mbuzi watatu wa maziwa. Kwa bahati mbaya, mmoja alikufa,” asema mkulima huyo, ambaye pia ni mwanachama wa kundi la Huruma Town Youth Group, linaloendesha shughuli za kilimo mtaa wa Huruma.

“Nilipoteza wazazi wangu kwa kukosa uwezo wa kupata lishe bora, jinsi walivyoagizwa na daktari. Njia nyingine ya kupata lishe ni kupitia kwa maziwa ya mbuzi, ambayo yasingepatikana kwa wakati huo katika vituo vya biashara. Hili likawa akilini mwangu nikiwa na matumaini kwamba siku moja ningepata suluhu ya tatizo hilo,” aeleza mkulima.

Baadaye, akawanunua mbuzi watatu wa maziwa kutoka Dagoretti, kutoka kwa afisa mmoja wa kilimo, kwa Sh12,000, Sh8,000 na wa kike kwa Sh25,000.

Yeye hukitumia kibanda chenye vipimo vya futi 24 kwa futi 12.

Anaongeza kuwa lishe anazozitumia kuwalisha mbuzi wake ni zile zinazokusanywa sokoni, lishe aina ya ‘hay’, majani ya mwarubaini na lishe za madukani.

Mfugaji huyo anasisitiza muhimu wa kusafisha mahali ambapo mbuzi hulala. Aidha, anaongeza kuwa, lishe zafaa kukaguliwa vyema kabla hazijaliwa na mbuzi.

Kwa wakati huu ana mbuzi 27, pamoja na wanambuzi 6 waliozaliwa siku chache zilizopita. Mkulima huyo huwakama mbuzi 6 kwa sasa.

Anafichua kuwa, hupata maziwa lita 8 kwa siku moja, japo anatarajia yaongezeke.

Kevin Uduny akionyesha baadhi ya bidhaa za maziwa ya mbuzi wanazotengeneza katika shamba la Toggfarm, Mathare, Nairobi. PICHA | PETER CHANGTOEK

“Baada ya kuzaa, mbuzi huwa na maziwa kidogo, lakini muda unavyosonga, maziwa huongezeka,” adokeza Uduny.

Anafuga mbuzi aina ya Alpine, Saanen na Toggenburg.

Mbali na kuuza maziwa ya mbuzi, mkulima huyo hutengeneza maziwa gururu; nusu lita ya maziwa gururu kwa Sh300-Sh350.

Pia, hutengeneza jibini (cheese) na kuuza gramu 100 ya jibini kwa Sh200-Sh250. Aidha, mkulima huyo huyauza maziwa ya mbuzi ambayo hayajaongezewa thamani kwa Sh150-Sh300 kwa lita moja.

Miongoni mwa changamoto ni bei ya juu ya lishe, maradhi na nafasi ndogo ya kufuga mbuzi wake.

magonjwa, japo anasema hayajawaathiri mbuzi wake, ajali na ukosefu wa nafasi ya kutosha ukosefu wa huduma za matibabu ya mifugo zilizo nafuu.

Baadhi ya magonjwa ambayo huwaathiri mbuzi ni yale yanayoathiri matiti, nimonia, pepopunda, miongoni mwa mengineyo. Anasema kuwa, ufugaji wa mbuzi wa maziwa huhitaji nafasi ndogo ya kuendeleza shughuli yenyewe.

“Ufugaji wa mbuzi ni rahisi kutekelezwa ikilinganishwa na ufugaji wa ng’ombe, kwa sababu huhitaji sehemu ndogo.

“Maziwa ya mbuzi yana virutubisho ikilinganishwa na maziwa ya ng’ombe. Mtu anafaa kufanya utafiti kabla hajaanza kufuga mbuzi,” asema Uduny.

Uduny, ambaye ni mwanachama wa Huruma Youth Group, anasema kuwa, wanachama wa kundi hilo hushughulika na usafishaji mazingira, ufugaji wa kuku, ufugaji wa mbuzi, njiwa, bata na hukuza mboga.

“Mipango yangu ya siku za usoni ni kuwa na shamba ili kuweza kuendeleza shughuli mbalimbali za kilimo na uchakataji, ili kupata mapato mazuri na kuwaajiri vijana wengi,” afichua Uduny.

Mbali na kuuza maziwa ya mbuzi, mkulima huyo hutengeneza maziwa gururu, na kuuza kwa nusu lita ya maziwa gururu kwa Sh300-Sh350.

Pia, hutengeneza jibini (cheese) na kuuza gramu 100 ya jibini kwa Sh200-Sh250. Aidha, mkulima huyo huyauza maziwa ya mbuzi ambayo hayajaongezewa thamani kwa Sh150-Sh300 kwa lita moja.

You can share this post!

Ukikutana na hizi ‘kanda mbili’ utajua ni za...

Mtambo unaochemsha na kuhifadhi maziwa yakisubiri kupata...

T L