• Nairobi
  • Last Updated May 16th, 2024 8:50 PM
Mapenzi yamewatesa sana mastaa hawa, na hivi ndio wameamua kufanya…

Mapenzi yamewatesa sana mastaa hawa, na hivi ndio wameamua kufanya…

NA SINDA MATIKO

“NIMEAMUA kuupumzisha moyo wangu maana siku nyingi unateseka juu yangu. Kutwa kupelekwa puta na akili yangu eti kisa kuuridhisha mwili wangu… Aah! Acha nikajaribu kwingine sio fungu langu pengine, moyo sukuma damu si vingine…”

Ndio mistari ya kwanza ya hiti yake Lameck Ditto aliyoiachia miaka sita iliyopita. Inawezekana Ditto aliutunga wimbo huo kutokana na matukio yaliyomkuta. Lakini hata kama hayakumkuta yamewakuta wengi sana na pia mastaa hawajasazwa.

OTILE BROWN

Baada ya kuvuruga sana mitaa akitoka na wanawake kadhaa akiwemo soshiolaiti Vera Sidika, ilifikia wakati watu wakaamini ametulia alipompata mrembo kutoka Ethiopia, Nabayet.

Utakumbuka penzi lao lilikuwa zito kiasi cha jamaa kusafiri mara kwa mara kumcheki mrembo wake. Penzi lilikuwa tamu kiasi cha jamaa kutoa nyimbo ‘Nabayet’ akimsifia mtoto wa watu.

Lakini penzi lao lilikumbwa na misukosuko kibao. Walijaribu tena kufufua penzi lao lakini baada yao kushindwa kufanya hivyo, kila mmoja aliamua kushika hamsini zake. Baadaye Otile aliamua kukaa singo akidai kuwa kumpata demu wa kweli hasa kwa mtu kama yeye ambaye ni staa, sio rahisi

BETTY KYALO

Kuna kipindi maisha yake hayakuwa yakifuatiliwa sana. Alipokuwa mtangazaji wa TV. Ila alipoamua kuaachana na utangazaji, watu walianza kupata kumjua Betty kivingine. Alianza kuyaanika maisha yake.

Toka ndoa yake kwa mwanahabari mwenzi Dennis Okari ilipovunjika baada ya miezi sita tu, mrembo huyo kavumishwa kutoka na wanaume kadhaa ikiwemo mwanasiasa Ali Hassan Joho, Somali bae, wakili Nick Ndeda na wengine kibao.

Hata hivyo, mahusiano hayo yote yalivunjika.

“Wajua kwenye mapenzi huwezi kuchagua utakayempenda. Kwa sasa nimeamua kuishi maisha haya ya kuwa solo. Nafurahia nafasi hii niliyo nayo ya kuwa singo. Ndio kuna wanaume wanaonifukuzia lakini kwa sasa acha nikae hivi. Nimegundua nimekuwa nikitumia nguvu nyingi sana kwenye kupenda. Sasa nataka kuelekeza nguvu hizo kwenye biashara zangu,” Betty kasema.

Lakini pia alikiri kuwa wanaume wengi humchukulia kama maua jambo ambalo limekuwa likimsinya na pia limechangia yeye kuamua kukaa singo.

DADDY OWEN

Toka ile drama iliyomkuta miaka miwili iliyopita anayodaiwa kukimbiwa na mke wake wa zaidi ya miaka mitatu Faridah Wambui, hali yake Owen ilikuwa mbaya sana.

Aliugua sonona na hata kupelekea muziki wake kushuka. Sijui mara yako ya mwisho kusikia hiti kutoka kwake ilikuwa lini?
Tangu akimbiwe na mke wake wa ndoa, Owen ameishi maisha ya upweke. Kwa sasa ameshaizoea hali hiyo na anasema, hana haraka tena kuwa kwenye mahusiano.

“Watu wanauliza kama ninadeti tena, kama ninapanga kuoa tena. Jibu langu ni, hapana. Kwa nini? Nahisi unapovunjwa moyo kwa kiasi kama kile, huwafanya watu kubeba mzigo mzito wa hisia kwa muda na hii inaweza kuwa hatari katika mahusiano mapya. Katika hali kama hii, unamwachia Mungu akuongeze,” kaka aliwahi kusema hivi karibuni.

JACKIE MATUBIA

Baada ya kumtimua aliyekuwa mpenzi wake mwigizaji mwenza Blessing Lungáho, Matubia kakiri kuwa kwa sasa hana muda na mapenzi tena.

“Nguvu zangu kwa sasa nazielekeza kwenye kuwalea wanangu na kujipenda mimi, wanaume hawaeleweki,” alifunguka majuzi.

EDDIE BUTITA

Aliachana na mpenzi wake wa miaka mingi mchekeshaji mwenza Mamitto Butita, na anasisitiza kuwa hana pupa ya kumpata mpenzi mwingine.

Kwa sasa msela anasema yeye anachowaza ni kutafuta hela na kuijenga kampuni yake ya SPM Buzz inayohusiana na habari za burudani.

  • Tags

You can share this post!

Wauzaji bangi wanavyotumia magari ya kifahari kuisafirisha

Pigo jingine kwa Serikali korti ikizima kesi dhidi ya...

T L