Na RICHARD MUNGUTI
SERIKALI imepata pigo tena baada ya mahakama kuu kusitisha kesi ya ulaghai wa Sh29 milioni aliyoshtakiwa Msimamizi wa Bajeti Margaret Nyakang’o Jumanne jijini Mombasa.
Akisitisha kusikizwa kwa kesi hiyo, Jaji Enock Chacha Mwita alisema kesi aliyowasilisha Bi Nyakang’o iko na mashiko kisheria.
Jaji Mwita alisitisha kusikizwa kwa kesi hiyo hadi Mei 21 2024 na kumwamuru wakili Danstan Omari aliyewasilisha kesi hiyo akabidhi Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) nakala za kesi hiyo katika muda wa siku 14.
Jaji huyo aliratibisha kesi hiyo kuwa ya dharura na kuamuru DPP ajibu malalamishi ya Bi Nyakang’o katika muda wa siku 14.
“Baada ya kusikiza mawasilisho ya mlalamishi Bw Stephen Mogaka (Mbunge wa Mugirango Magharibi) na wakili Bw Omari nimefikia uamuzi kwamba haki za Bi Nyakang’o zimekandamizwa,” Jaji Mwita alisema.
Jaji huyo alisema kuna masuala nyeti ya sheria anayozua pamoja na kudai haki zake zimekandamizwa.
Katika mawasilisho yake, Bw Omari alisema kukamatwa na kushtakiwa kwa Bi Nyakang’o kunamfedhehesha.
Msimamizi huyo wa bajeti alikamatwa na kushtakiwa mbele ya hakimu mkuu wa Mombasa kwa ufisadi wa Sh29 milioni.
Alikana mashtaka na kuachiliwa kwa dhamana ya Sh500,000.
Alishtakiwa kwamba alimlaghai Bi Claudia Mueni Mutungi Sh29 milioni kwa kughushi sahihi yake akidai atanufaika katika uwekezaji kwenye chama cha ushirika cha FEP Sacco Advantage (Mavuno) kati ya Novemba 1 2019 na Mei 2020.