NA FRIDAH OKACHI
MWANAMITINDO Milka Mukami amesafiri kuelekea nchini Ufilipino kwa shindano la urembo.
Shindano hilo la wanamitindo litaanza rasmi Oktoba 1-9, 2023. Mataifa mbalimbali kote duniani yatakuwa na wawakilishi.
Mwanamtindo huyo atakuwa anawakilisha taifa la Kenya kwa mara ya arubaini na sita.
Bi Tinah Lughano ambaye ni msimaminzi wa shirika la Mrs Universe Pageant, aliambia Taifa Leo kuwa Bi Mukami atakuwa anawakilisha taifa la Kenya kwa vitengo kadhaa, kimojawapo kikiwa ni utalii, utamaduni, urithi, biashara na sanaa.
Shirika la Pageant huwasherekea wanawake wa kati ya umri wa miaka 18 hadi 55 ambao wana familia, kazi na wanajihusisha na miradi ya kuifaa jamii.
“Mwaka huu, shindano hili linashirikisha wanamtindo 120. Miongoni mwao ni Bi Mukami. Ni kweli Bi Mukami amesafiri mapema leo kuelekea nchini Ufilipino. Tuna tumaini kuwa atakuwa mshindi,” alisema Bi Lughano.
Mwaka 2022 taifa la Kenya lilikuwa miongoni mwa 18-bora baada ya Bi Mukami kuwakilisha taifa lake.
Bi Mukami alikuwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Daystar. Taaluma yake ni mawasiliano. Kando na urembo anaofahamika nao, anatambulika kwa masuala ya amani na kutatua mizozo.
Mwanamtindo huyo ana mradi wa “Healing Healers” unashirikisha wanawake wanaopitia dhuluma katika jamii. Mradi huo ukiwaleta pamoja wanawake walio kwenye vyama na kuwaelimisha kuhusu dhuluma za kijinsia.