• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 7:50 AM
Mwigizaji Bwire Ndubi aomba msaada wa kifedha kupata matibabu spesheli

Mwigizaji Bwire Ndubi aomba msaada wa kifedha kupata matibabu spesheli

NA FRIDAH OKACHI

MWIGIZAJI katika kipindi cha Sultana Bwire Ndubi almaarufu ‘Dida’, anaomba msaada wa kumsaidia kuchangisha Sh7 milioni zitakazotumika kwa kusafiri na kutafuta matibabu maalum ya saratani nje ya nchi.

Kupitia kwenye ukurasa wake wa Instagram, mwigizaji huyo anataka kuokoa maisha yake baada ya kupambana na saratani ya matiti inayofahamika kama Metastatic ambayo kwa muda wa miaka miwili bado hajapona.

“Ombi langu ni sikukuu ya Krismasi ifike vizuri. Ninakuja kwako, kutafuta msaada wa kunisaidia kupata matibabu spesheli nje ya nchi katika juhudi za kuokoa maisha yangu,” aliandika Dida.

Dida aliongeza kuwa hali hiyo imemfanya kupambana na pepo ambaye hakuwahi kufikiria angekutana naye maishani mwake.

Mwigizaji huyo alijipa tumaini na imani kuwa wasamaria wema watamsaidia kuokoa hali yake ya afya ambayo kwa sasa imedorora.

“Je, maisha ni ghali kiasi gani? Dakika moja unaishi maisha mazuri ya kutamanika na dakika inayofuata unakumbana na pepo ambaye hukuwahi kufikiria kuwa ungekutana naye katika maisha yako yote,” akafunguka Dida.

Aliwaomba mashabiki wake na wote wanaoguswa kusimama naye katika safari ya kutafuta matibabu.

“Nichangieni chochote muwezacho ili kunisaidia kufikisha Sh7 milioni zinazohitajika. Msaada wa kila mmoja wenu utathaminiwa,” alisema mwigizaji huyo.

Saratani yake ilianza na dalili za uvimbe na alipomtembelea daktari, alimjulisha kwamba alikuwa na maambukizi ya jumla na alipewa dawa za kupunguza uvimbe.

Uchunguzi huo ulitambua kuwa ana aina ya saratani adimu inayohusisha kuwepo kwa seli zisizo za kawaida kwenye titi.

  • Tags

You can share this post!

Polisi wawinda wahalifu waliovamia dukakuu la Shivling

Mwanamume apatikana amefariki mwili wake ukining’inia...

T L