• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 2:31 PM
Chimbuko na Asili ya lugha ya Kiswahili

Chimbuko na Asili ya lugha ya Kiswahili

NA CHRIS ADUNGO

WATAALAMU wa lugha wanakadiria kuwa idadi ya wazungumzaji wa Kiswahili kote ulimwenguni imefikia zaidi ya watu milioni 250.

Hata hivyo, lugha hii hutumiwa na watu wengi katika pembe nyingi za dunia bila kufahamu chimbuko wala asili yake. Zipo nadharia kadhaa kuhusu asili ya Kiswahili – kuwa Kiswahili kimetokana na Kiarabu; kuwa ni mchanganyiko wa Kiarabu na lugha za Kibantu; na kuwa ni lugha ya Kibantu iliyoathiriwa sana na Kiarabu kimsamiati.

Wengine wamedai kuwa Kiswahili kilitokana na mchanganyiko wa lugha kadhaa za Kibantu zilizokuwa katika upwa wa Afrika Mashariki.

Nadharia kuwa Kiswahili kilitokana na Kiarabu inaegemea sana wingi wa maneno yenye asili ya Kiarabu na dini ya Kiislamu. Inadaiwa kwamba kwa kuwa Kiswahili kilianzia pwani, na kwa kuwa idadi kubwa ya wakazi wa pwani ni Waislamu, na kwa kuwa Uislamu uliletwa na Waarabu; basi Kiswahili nacho kinashabihiana na Kiarabu.

Hata hivyo, madai haya hayana mashiko yoyote kwani Kiswahili ni lugha kamili ya Kibantu iliyokopa maneno kutoka kwa Kiarabu, Kiajemi, Kireno, Kihindi, Kijerumani, Kiingereza n.k kutokana na mawasiliano ya karne nyingi kati ya wenyeji wa pwani na wafanyabiashara wa kigeni.

“Mabadiliko yalihusu msamiati tu wala si maumbo ya maneno au miundo ya tungo za Kiswahili. Kiswahili kilitumia maneno mengi kutoka lugha za Kibantu kwa kuwa wasemaji wengi wa Kiswahili ni Wabantu,” anasema Prof Joseph Nyehita Maitaria wa Chuo Kikuu cha Karatina, Kaunti ya Nyeri.

“Lugha kuwa na maneno mengi ya kukopa kutoka lugha fulani si ithibati kwamba lugha hiyo imetokana na nyingine. Inabidi kuzingatia zaidi msingi wa lugha kwa vigezo vya kiisimu – fonolojia, mofolojia, sintaksia na semantiki,” anasisitiza mtaalamu na mtafiti wa Kiswahili, Bw Abdurahim Ali Bakathir.

Vipengele ‘vinavyohalalisha’ nadharia kuwa Kiswahili ni Kibantu ni ushahidi wa kiisimu na wa kihistoria. Kiisimu, Kiswahili kina utaratibu maalumu wa sauti za irabu na (au) konsonanti katika kuunda silabi, maneno, n.k.

Pwani

Watu wa kwanza kufika pwani ya Afrika Mashariki ni makabila mawili ya jamii ya Wangozi – Wabarawa (Wamiini) waliotumia lahaja ya Chimbalazi na Wabajuni (Watikuu) kutoka Shungwaya.

Wangozi walitokea mjini Harar, Ethiopia Mashariki. Walianza kuitwa Waswahili baada ya kufikiwa na mgeni Muhammad Ibn Battuta aliyesema “hawa watu ni wa fukwe za pwani” akilenga Wa-Amu kwamba ndio wenye lugha ya Kiswahili.

Kwa hivyo, si kweli kwamba Waswahili wamezaliwa na Wamijikenda kwa sababu Wamijikenda walitokea Afrika ya Kati na wakakaribishwa na Waswahili pale Shungwaya. Kihistoria, nchi ya Waswahili (Swahililand) ni maili 12 kutoka ufukwe wa pwani kupanda juu bara na kuanzia Lunga-Lunga hadi mji wa Mogadishu, Somalia.

“Waswahili ni jamii ya makabila 17 ambayo yamepasua kingo kutoka pwani na kuenea katika sehemu mbalimbali kisha kupanua mawanda na maana ya ‘Mswahili’. Sasa tuna Waswahili asili, wazawa na waridhiwa wanaoelewana kilahaja,” anaeleza Bakathir.

Kuna maneno mawili tunayochanganya katika matumizi nayo ni, asili ya Kiswahili na chimbuko lake. Neno ‘asili’ lina maana ya jinsi jambo lilivyoanza au lilivyotokea. Neno ‘chimbuko’, maana yake ni mahali kitu au jambo lilipoanzia. Kwa hivyo asili na chimbuko yanatofautiana katika maana.

Ni vigumu kusema kwa uhakika mahali ambapo ni chimbuko la Kiswahili. Pengine tunaweza kusema kuwa Kiswahili kilianzia sehemu maalumu na kuenea hadi mahali fulani. Inadaiwa kuwa chimbuko la Kiswahili ni katika maeneo ya Kaskazini Mashariki mwa Kenya lakini madai haya hayajawahi kuthibitishwa kwa hoja zenye mashiko.

Ni wazi kuwa wanahistoria waliowahi kuandika kuwa mawasiliano na maelewano kati ya watu wa eneo fulani kwa kiasi fulani kulizuka lugha moja iliyoeleweka kwa watu wote katika eneo hilo. Mawasiliano ya aina hii yalizua lugha ambazo zilitofautiana kuanzia Kaskazini hadi Kusini mwa Pwani ya Afrika Mashariki ambazo zilijulikana kama lahaja za Kiswahili. Lahaja hizi zinafanana na lugha nyinginezo za Kibantu. Lahaja hizi zinatofautiana kidogo na Kiswahili sanifu kwa sababu Kiswahili sanifu kina maneno mengi ya mkopo. Lahaja zote hizo ni lugha zinazojitegemea.

  • Tags

You can share this post!

Julai 7: Siku ya Kiswahili Duniani

Hatimaye Uganda yakweza Kiswahili kuwa lugha rasmi

T L