• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 10:48 AM
Corona ilivyoyasukuma makanisa kuchangamkia teknolojia

Corona ilivyoyasukuma makanisa kuchangamkia teknolojia

Na MWANGI MUIRURI

Athari za ugonjwa hatari wa Covid-19 zimechangia kusukuma makanisa hadi kukumbatia Tenknolojia za kimawasiliano (IT) kuwafikia waumini wao wanaozidi kuzimwa kufika kanisani.

Huku awali wahubiri wengi wakitumia mitandao ya facebook, Twitter, WhatsApp na jumbe za moja kwa moja hadi kwa simu za mikononi mwa waumini, hali imebadilika baada ya kutambuliwa kwamba sio washirika wengi huwa na uwezo wa kununua simu mwafaka za kuingia katika intaneti na ikiwa wako nazo, uwezo wa kununua mbado za data au ufahamu wa kutegea mahubiri hayo ni finyu sana.

Ndipo wahubiri wanang’ang’ana sasa kusajili vituo vya radio na pia runinga ili kuwawezesha kuwafikia waumini katika manyumba yao.

Hapo ndipo sasa ushindani mkuu wa Kunasa washirika uko kwa kuwa kufungulia runinga au radio hakuna ule utiifu wa imani kwamba ikiwa Basi kanisa langu haliko angani kunihubiria basi sitawasikiliza wale wanaonifikia.

Tayari, kuna zaidi ya vituo 15 vya runinga ambavyo vimezinduliwa na makanisa huku pia kukiwa na zaidi ya vituo 10 vya radio vya kuwafikia washirika.

Wale ambao hawajaweza kuzindua runinga au radio wamenunua nafasi katika vyombo vya habari hapa nchini ya kuwawezesha Kutoa mahubiri yao.

Kanisa la Kipresibeteria hapa nchini (PCEA) tayari limeelekeza matawi yake yote yaliyo katika Kaunti za Nairobi, Kiambu, Kajiado, Nakuru na Machakos yazindue misa za kimitandao ambapo linawataka wachungaji wao wawe wabunifu katika kuwafikia washirika wao.

Hii ni baada ya Kutoa amri pia makanisa hayo yote ndani ya hizo Kaunti tano yasistishe ibada zao zote mara moja kwa mujibu wa amri ya rais Uhuru Kenyatta.

Alhamisi, rais aliorodhesha kaunti hizo tano kuwa zilizoambukiwa kwa kiwango kikuu maradhi ya Covid-19 yanaosababishwa na virusi vya Corona na kwa kutii ushauri wa wataalamu wa Kiafya, akaziwekea vikwazo vgya kutangamana.

Katika amri yake, rais alisitisha kuingia au kutoka kwa Kaunti hizo ambazo zote ziko katika mduara mmoja wa ujirani lakini akawakubalia wao wenyewe kutembeleana akisema kufanya hivyo ni kusaka mbinu ya kuzima uenezaji hadi mashinani ya kwingine nchini kupitia shughuli za uchukuzi.

Rais Kenyatta aliambatanisha amri hiyo na kuzima ibada zote za makanisa katika mduara huo wa Kaunti tano, sasa kanisa hili la PCEA likitii na kuwaelekeza wachungaji wake wazindue mikakati ya kuwafikia waumini wao kupitia njia za kiteknolojia.

Misa zote zitaathirika na amri hiyo ambapo hata wale watoto ambao hushiriki misa za ukombozi, utakaso na ubatizo wataahirisha harakati hizo hadi ushauri mwingine wa kufutilia mbali makataa hayo utolewe.

Katika barua iliyoandikwa na Kaimu Katibu Mkuu wa PCEA Askofu Paul Kariuki na kisha kutumwa kwa dayosesi zote za Kanisa hilo, ilisema kuwa pia ni lazima makanisa yote yake nchini yazingatie amri ya awali ya rais kuwa idadi ya watakaokuwa wakifika makanisani katika Kaunti zingine 42 ambazo hazikuathirika na makataa ya usafiri iwe ni asilimia 30 pekee.

Waumini wa kanisa hili ambao Taifa Leo iliongea nao waliunga mkono hatua hiyo wakisema watatii na waendelee kumuomba Mungu wakiwa katika makazi yao na pia walio na uwezo wakifuatilia misa katika mitambo ya kiteknolojia.

Nalo kanisa la Jesus Winner Ministries lake Askofu Edward Mwai likitangaza kuwa kuambatana na amri hiyo Rais Kenyatta, limeahirisha ibada makanisani katika Kaunti hizo tano.

“Ningewaomba washirika wetu wawe wakitegea mahubiri ya Askofu wetu kupitia runinga ya Mwangaza na pia kituo cha radio cha Mwangaza FM,” ikasoma taarifa kwa vyombo vya habari.

Ni amri ambayo inaonekana tayari kukumbatiwa na mengi ya maeneo ya ibada tayari tangazo sambamba na hilo likitoka kwa makanisa ya Kianglikana, AIPCA, ACC&S, Katoliki, Deliverance huku mengine yakitazamiwa Kutoa mwelekeo sawa na huo.

You can share this post!

Watu 45 walifariki katika makanyagano wakitazama mwili wa...

Mama Sarah Obama azikwa katika hafla iliyohudhuriwa na...