• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 4:10 PM
FUNGUKA: ‘Jikedume mambo yote’

FUNGUKA: ‘Jikedume mambo yote’

NA PAULINE ONGAJI

Mara kwa mara tumekuwa tikisikia jinsi mojawapo ya mbinu za kudumisha uhusiano au ndoa kama kama mke, ni kuwa mnyenyekevu na kumheshimu mumeo.

Wanaume wengi wanasemekana kuenzi amani katika uhusiano na nyumbani, na kamwe hawawezi kumstahimili mwanamke mkorofi.Lakini kwa Henry, mambo ni tofauti sana.

Yeye anavutiwa sana na mabinti wakorofi na wasio na nidhamu. Kwanza kabisa acha nikujuze kuhusu kaka huyu.Ana umri wa miaka 35 na kimasomo hakuenda mbali baada ya kukamilisha kidato cha nne takriban miongo miwili iliyopita.

Lakini licha ya hayo, alijiendeleza kibiashara na kuwekeza katika nyanja mbalimbali, ambapo ametumia mapato hayo makubwa kama jukwaa la kuanzisha safari yake kisiasa.

Amekuwa diwani kwa vipindi viwili, lakini msimu wa uchaguzi uliopita, alimua kupumzika kutoka siasa ili kunoa makali yake, ambapo anatarajiwa kurejea ulingoni katika uchaguzi mkuu ujao kuwania kiti cha ubunge.

Henry hana mke licha ya kufanikiwa kuchumbia mabinti kadhaa warembo. Inasemekana kwamba kizingiti kikuu ni masharti yake yasiyo ya kawaida inapowadia wakati wa kuwachagua wapenzi, kama anavyoeleza mwenyewe.

“Napenda mwanamke mwenye nguvu za kimwili, ambaye mbali na kuwa na mazoea ya kunikosea heshima kila mara kupitia ukorofi na matusi yake, pia anaweza kunipiga.Kwa hivyo mojawapo ya sifa ninazotafuta ninapomsaka mpenzi ni mwenye mwili mkubwa kuniliko.

Nikisema mwili mkubwa namaanisha kwamba lazima awe amenizidi kimo, na pia awe mnene zaidi kuniliko.Mwili huu mkubwa unamaanisha kwamba nikivimba kichwa anaweza nitandika mbaya.

Aidha, mwili huu mkubwa ni kinga kwangu kama mwanaume hasa mwanasiasa.Yuko tayari kuwatia adabu mabinti wanaojaribu kunikonyezea macho, na kwa upande wa siasa ni mlinzi wangu dhidi ya wapinzani.

Kitabia, lazima awe jeuri na mkorofi, yaani sio mwanamke mtiifu. Bibi ambaye yuko tayari kupinga na kukiuka maagizo yangu.Lazima anoe kinywa chake na kujifunza lugha chafu itakayowachana wapita njia kinywa wazi.Chumbani lazima anichangamshe kwa ukorofi, ujeuri na matusi yake ili kunipandisha ashiki.

Lazima awe mchangamfu na tayari kunitawala tukiwa chumbani. Yaano awe na nguvu za kutosha hata kunibeba wakati huu.Bila shaka niko tayari kumkubali binti asiye na sifa hizi, lakini je, ukipewa nafasi uko tayari kubadilika na kufuata mkondo niutakao?

Kwa upande wa kimo tunaweza kukubaliana ila hayo mengine lazima uwe tayari kukumbatia. Kwa mfano, ukiwa mwembamba lazima utie bidii kuongeza uzani. Ukiwa u mpole kitabia, lazima uwe tayari kuongeza ukorofi na ujeuri, la sivyo nikuteme.

Japo nashuku kwamba hii ni mojawapo ya sababu ambazo zimefanya iwe changamoto kwangu kudumisha uhusiano, sibadili nia kamwe na kwa yeyote anayetamani kuwa mpenzi, mchumba au mke wangu, sharti akubaliane nami”.

You can share this post!

Serikali yaonya wasimamizi wa vyama vya kahawa

Mwilu mwanamke wa kwanza kuteuliwa kaimu Jaji Mkuu