NA CHRIS ADUNGO
NDOTO ya kuwa mwanamuziki ilianza kumtambalia Subiri Jay katika umri mdogo.
Wazazi wake walimruhusu ajiunge na makundi ya uimbaji kanisani na shule ya msingi ya Voi alikosomea ikampa fursa nyingi za kushiriki mashindano ya ngazi na viwango tofauti.
Alijiunga baadaye na kundi la ‘Wa Mungu’ lililomkuza zaidi kisanaa akiwa mwanafunzi wa shule ya upili ya Mwaghogho iliyoko Tausa, Voi, Kaunti ya Taita Taveta.
Kundi hilo lililojumuisha waimbaji, wasakataji densi na mafundi wa kucheza ala mbalimbali za muziki, lilitegemewa pakubwa kutumbuiza wanafunzi, walimu, wazazi na wageni nyakati za hafla na mikutano muhimu shuleni Mwaghogho.
Baada ya uchechefu wa karo kukatiza ghafla safari yake ya masomo ya sekondari mnamo 2013, Subiri alirejea nyumbani kufanya vibarua vya kila sampuli, ikiwemo kazi ya upishi katika mji wa Voi na eneo la Emali, Kaunti ya Makueni.
Mnamo 2017, alielekea jijini Nairobi na akajitosa kikamilifu katika sanaa ya muziki akishirikiana na msanii Hunderson Peter aliyekuwa mwanafunzi mwenzake katika shule ya msingi na upili. Alipata pia nafasi ya kucheza piano na ala nyinginezo za muziki katika Kanisa la ATG mjini Juja, Kaunti ya Kiambu.
Kufikia sasa, anajivunia zaidi ya nyimbo 20. Alitoa albamu ndogo (EP) iliyo na nyimbo sita, ‘Nitasimama’, mnamo Januari 2022 kisha akafyatua EP nyingine yenye nyimbo saba, ‘Life Like This’ miezi 10 baadaye.
Mtazamo
Kwa mtazamo wake, kazi iliyomkweza juu zaidi katika ngazi ya muziki ni kibao ‘Banjuka’ alichokitoa Disemba 2022 akishirikiana na waimbaji wa Tweletu Band pamoja na wasanii Moji Shortbabaa, Benachi, Abu Scatter na Pinto.
Kubwa katika maazimio yake kisanaa ni kuhifadhi nyimbo zake katika albamu na kuchomoa wimbo mpya kila atakapohisi ana ujumbe unaostahili kuipa jamii mwelekeo. Anapania vilevile kupanua wigo wake wa ujasiriamali mjini Voi anakomiliki studio ya kurekodi nyimbo.
Tangu Agosti 2022, Subiri amekuwa akitumia kipindi cha mitandaoni cha ‘Moment With Subiri Jay’ kueneza Ukristo na kuwaelekeza vijana wenzake kimaadili. ‘Soma’, ‘Subiri’, ‘Nakupenda’ na ‘Kiki’ ni nyimbo nyinginezo ambazo amezisana kwa Kiswahili.
Zaidi ya kushirikiana kikazi na wasanii Christina Shusho na Mercy Masika, matamanio yake mengine ni kutambua, kukuza na kulea vipaji vya wanamuziki chipukizi huku akiendelea kuachilia nyimbo zinazokubalika kimataifa.
Subiri alilelewa katika eneo la Voi, Taita Taveta. Ndiye wa sita kuzaliwa katika familia ya watoto saba wa Bw Jonas Muema na Bi Veronicah Kiasyo.
“Jifunze kutokana na yaliyopita ili ujenge ya sasa na kujiweka pazuri kukabili yajayo. Salia imara katika safari ya kufikia matamanio yako. Jiamini, mtumainie Mungu katika kila jambo na usichoke kutafuta,” anashauri.
Subscribe our newsletter to stay updated