• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 5:50 AM
Jinsi ya kuandaa pilau ya mboga mbalimbali

Jinsi ya kuandaa pilau ya mboga mbalimbali

Na MARGARET MAINA

[email protected]

Muda wa kuandaa: Dakika15

Muda wa mapishi: Saa 1

Walaji: 3

Vinavyohitajika

  • mchele wa kupikia biriyani kilo nusu
  • bizari nyembamba
  • njegere kikombe 1
  • majani ya giligiliani
  • vitunguu maji 2
  • nyanya 3
  • tangawizi iliyomenywa kijiko 1
  • punje 3 za kitunguu saumu
  • viungo vya pilau (chaguo lako)
  • karafuu kikombe nusu
  • pilipili
  • karoti 2
  • pilipili mboga
  • koliflawa

Maelekezo

Menya vitunguu maji na kata kufuatisha uviringo wake ili upate umbo la mduara kisha weka kwenye chombo.

Osha nyanya na kata vipande vinne kwa kila nyanya.

Osha karoti na kisha kwangua kiasi.

Osha na kisha kwangua kiasi cha karoti na nyingine kata vipande vidogo.

Osha koliflawa na itoe kwenye shina ili upate maua yake.

Osha majani ya giligiliani halafu uyakate.

Osha na weka njegere kwenye chombo chenye maji.

Menya tangawizi na kisha ikwangue.

Menya vitunguu saumu kisha uvitwange.

Andaa viungo vyote vya pilau pembeni tayari kutumika.

Osha na kisha andaa karafuu na pilipili.

Injika sufuria kwenye meko. Mimina mafuta ya kupikia. Weka viungo vya pilau vya unga kisha weka bizari na kaanga kwa muda kiasi.

Weka kitunguu saumu na ukoroge kiasi. Weka tangawizi na endelea kukoroga.

Weka kitunguu maji kisha koroga kwa muda kiasi. Acha viive hadi vianze kubadilika rangi.

Weka nyanya, chumvi, na pilipili manga. Koroga na kisha acha vichemke kwa dakika chache.

Weka karafuu, karoti, pilipili mboga, koliflawa na njegere. Endelea kukaanga kwa muda wa dakika kama 10 hivi.

Weka mchele huku ukiendelea kukaanga ili mchele wako uchanganyike vizuri na viungo kwenye sufuria ukiiva.

Weka maji kulingana na kiasi cha mchele wako unaoanza kuiva.

Weka moto wa wastani na kisha funika sufuria chakula kiive. Baada ya robo saa, geuza pilau kisha weka majani ya giligiliani ili kuongeza ladha na harufu nzuri ya chakula. Funika chakula ili kiendelee kuiva.

Subiri kwa muda wa dakika 10 na chakula kitakua tayari kuliwa.

Pakua na ufurahie.

You can share this post!

Polo ajuta kutafuna kuku na mayai yake

Tatizo la tumbo kujaa gesi na jinsi ya kukabiliana na hali...